×

Aslay afunguka kujiunga Wasafi

KWA mara ya kwanza, staa wa Bongo Fleva, Aslay Isihaka Nassoro amefunguka juu ya tetesi za muda mrefu kwamba, yupo kwenye mipango ya kujiunga na Lebo ya Wasafi Classic Baby (WCB) inayomilikiwa na mwanamuziki Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’.  Aslay amefikia uamuzi wa kueleza ukweli wake juu ya ishu hiyo akiwa kwenye ziara ya kuitangaza EP (Extended Play; nyimbo kadhaa kabla ya albam) yake inayokwenda kwa jina la Kipenda Roho huko nchini Kenya.

Akihojiwa na televisheni moja nchini humo wikiendi iliyopita, Aslay alifunguka mengi ikiwemo namna ambavyo amefanikiwa kuzunguka kwenye vyombo vingi vya habari nchini humo. Kama ulikuwa hujui, tangu kuvunjika kwa Yamoto Band, Aslay amekuwa akihusishwa kujiunga na Wasafi huku mwenyewe akiendelea kuachia nyimbo kila kukicha na kuendelea kushika chati za juu. Mtangazaji wa televisheni hiyo alimuuliza Aslay;

“Kwa muda mrefu kumekuwa na tetesi kuwa WCB walikutafuta wakitaka kukuchukua kwenye Lebo ya Wasafi, je, ni kweli? Na ni kitu kinaweza kutokea?” Kwa upande wake Aslay alijibu; “Si kweli! Lakini mimi ni msanii na chochote kinaweza kutokea, cha muhimu tukae chini tuelewane, basi. “Mimi ni msanii, natafuta hela, so ikitokea wananihitaji ndipo tutakaa na kuelewana.”

Hata hivyo, suala ambalo Gazeti la IJUMAA WIKIENDA linalifanyia kazi ni uwepo wa madai ya kuwa, baadhi ya wasanii wamekuwa wakiogopa kujiunga na lebo hiyo baada ya Harmonize kusema alitoa shilingi milioni 500 ili kuvunja nayo mkataba alioingia mwaka 2016.

Leave a Comment