
STELLA IMMANUEL ni daktari ambaye amekuwa chanzo cha mkanganyiko kuhusu madai ambayo hayajathibitishwa kuhusu dawa ya malaria kuwa na uwezo wa kutibu Covid- 19.
Facebook na Twitter zimeondoa video ambayo daktari huyo alikuwa akionekana, makampuni hayo yakisema kuwa video hiyo imekiuka sera ya taarifa za kupotosha- lakini kabla ya hayo ilikuwa imechapishwa tena na Donald Trump na mmoja wa watoto wake wa kiume.
Rais wa Marekani alijitetea, pia akimsifu daktari huyo mzaliwa wa Cameroon na aishiye mjini Houston jimbo la Texas.
Trump alisema: ”Alisema amepata mafanikio makubwa baada ya kuwatibu mamia ya wagonjwa wa Covid-19, nilifikiri sauti yake ni sauti muhimu lakini sijui chochote kumhusu,” alisema siku ya Jumanne.
Dkt Immanuel, ambaye pia ni mchungaji, alitoa hotuba kuhusu hatua za mahakama ya juu ya Marekani iliyo jijini Washington, huku akipigwa picha ya video ambayo kwanza ilichapishwa kwenye tovuti ya Breitbart siku ya Jumatatu.
Sambamba na madaktari wengine kutoka taasisi ya madaktari wa mstari wa mbele nchini Marekani, alisema kuwa Wamarekani wamekuwa wakizuiwa kutumia dawa muhimu kwa ajili ya tiba ya Covid-19.
”Hakuna anayetaka kuugua. Virusi hivi vina tiba — inaitwa hydroxychloroquine, nimewatibu wagonjwa zaidi ya 350 na hakuna kifo hata kimoja kilichotokea,” alisema Dkt Immanuel.
Pamoja na tafiti za awali kutoa matumaini kuwa dawa hiyo ingeweza kutumika kutibu virusi vya corona, jaribio kubwa lilifanyika na kuonyesha kuwa haina ufanisi kama tiba.
Shirika la afya duniani (WHO) limesimamisha majaribio yake, likisema kuwa dawa hiyo haipunguzi viwango vya vifo kwa wagonjwa wa corona.

Mwezi uliopita, mamlaka ya Chakula na Dawa ya Marekani (FDA) ilitahadharisha dhidi ya matumizi ya dawa katika kutibu wagonjwa wenye virusi vya corona, baada ya kuwepo kwa ripoti kuwa ” imekuwa ikisababisha matatizo ya moyo” na matatizo mengine ya kiafya.
Na Dkt. Anthony Fauci, kiongozi wa kikosi kazi cha Ikulu kinachopambana na virusi vya corona, amerejea kauli hii.
”Tunajua kila utafiti mzuri umeonyesha kuwa hydroxychloroquine haina ufanisi katika tiba ya Covid -19,” aliliambia BBC siku ya Jumatano.
Lakini Dkt Immaniel amesisitiza kuwa kumeza hydroxychloroquine hakuna madhara kwa kuwa kwa kiasi kikubwa inatumiwa nchini mwake Cameroon, ambako kuna ugonjwa wa malaria.
Dkt Immanuel ni nani?
Alizaliwa mwaka 1965 na kuhitimu shahada ya kwanza ya tiba kutoka Chuo Kikuu cha Calabar nchini Nigeria na ana leseni ya utabibu, kwa mujibu wa tovuti ya bodi ya kitabibu ya Texas.
Pia ni mchungaji na muanzilishi makanisa Houston, jukwaa ambalo amelitumia kunadi mawazo yake mengine juu ya taaluma ya matibabu. Mahubiri yake yako katika akaunti ya mtandao wa YouTube uliofunguliwa mwaka 2009.
Miaka mitano iliyopita, alidai kuwa kipimo cha vinasaba cha DNA cha viumbe wanaodhaniwa kuishi katika dunia nyingine (aliens) vinatumiwa katika dawa za matibabu na kwamba wanasayansi wanatengeneza chanjo ya kuwazuia watu kuwa wafuasi wa dini.

Uchawi na mashetani
Baadhi ya madai yake mengine ni pamoja na kusema kuwa baadhi ya matatizo ya kiafya yamesababishwa na uchawi na mashetani – jambo ambalo kwa kawaida linaaminiwa miongoni mwa baadhi ya wahubiri wa Kikristo — ingawa anasema kuwa mashetani hayo hufanya ngono na watu kupitia ndoto.
“Wanageuka kuwa wanawake halafu wanalala na wanaume na kukusanya mbegu zao za kiume…halafu wanageuka kuwa wanaume na kulala na mwanaume na kuingiza mbegu zao za kiume na kuzaana kwa wingi ,” alisema wakati wa mahubiri mwaka 2013.
Suala jingine ni kwamba Dkt Immanuel huzishambulia ndoa za watu wa jinsia moja, akisema kuwa inaweza kusababisha watu wazima kuwaoa watoto, kwa mujibu wa gazeti la Daily Beast.
Pia huwaombea watu kuondoa mikosi ya kifamilia, ambayo walipokea kutoka kwa mababu zao, waliyoipata kupitia kondo la nyuma, unasema utambulisho wa tovuti yake.

‘Yesu atafunga Facebook’
Katika ukanda wake wa video uliotumwa hivi karibuni katika ukurasa wa Twitter Jumanne wiki hii, aliwaomba wagonjwa ambao anasema aliwaponya Covid-19 kujitokeza hadharani.
“Kama hutazungumza tunakwisha ,” alisema, huku akiwaomba watumie kampeni ya mtandaoni kwa alama ya reli (hashtag) wakati alipotuma jumbe zao za video.
Ujumbe wake wa Twitter ulishirikishwa zaidi ya mara 27,000
Baada ya kampuni ya Facebook kuondoa video ya Dkt huyo wa wagonjwa wa corona Jumanne, alitangaza kuwa Yesu ataangamiza mtandao huo mkubwa wa kijamii kama video zake hazitarudishwa tena mtandaoni. Facebook bado haijajibu juu ya hatua hiyo yake ya kuondoa video hiyo.