×

JPM Aeleza Dhamira Kugombea Urais -(Video +Picha)

Mgombea urais waChama Cha Mapinduzi  (CCM) Rais John Magufuli akizungumza na viongozi, wanachama na wapenzi wa chama hicho katika makao makuu ya chama hicho jijini Dodoma baada ya  kuchukua fomu ya urais.

SIKU moja baada ya pazia la uchukuaji fomu za urais kufunguliwa na Tume ya Uchaguzi (NEC) leo mgombea urais was Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais  John Magufuli amechukua fomu hiyo katika ofisi za tume hiyo Njedengwa jijini Dodoma.

Baada ya kuchukua fomu hiyo, alienda katika ofisi za Makao Makuu ya CCM (White House) na kuzungumza na viongozi, wanachama na wapenzi wa chama hicho ambao walijitokeza kumlaki.

Mgombea Mwenza wa urais wa CCM, Samia Suluhu Hassan, akizungumza na wanachama wa chama hicho Makao makuu ya CCM Dodoma.

Magufuli ameongozana na mgombea mwenza wake ambaye ni Makamu wa Rais,  Samia Suluhu Hassan, Katibu Mkuu wa CCM, Bashiru Ally, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Spika wa Bunge Job Ndugai na viongozi wengine wa sekretarieti na jumuiya za chama hicho.

Akizungumza na wanachama waliojitokeza kumlaki  amesema amechukua fomu ya kugombea urais kwa mara ya pili ili aweze kumalizia kazi ya kuwatumikia Watanzania kwa miaka mingine mitano huku akisema kampeni za chama hicho zitazinduliwa katika Jiji la Dodoma ambapo ndipo makao makuu ya nchi.

 Magufuli na  Samia Suluhu Hassan wakimkabidhi Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma fomu za udhamini kwa ajili ya kuomba wadhamini wa kuwadhamini mkoani Dodoma.

Ameyataja mafanikio ambayo serikali yake imeyapata kuwa ni pamoja na kuboresha huduma za afya kwa kujenga vituo vya afya zaidi ya 500, Shule za Msingi na Sekondari, umeme kila kijiji sambamba na ujenzi wa barabara za lami ambazo zimerahisisha huduma mbalimbali za kijamii.

Ameongeza kwamba  leo Tanzania imefikia uchumi wa kati baada ya kazi kubwa ambayo serikali yake imefanya kwa kuwabana mafisadi na kuzuia mali za Tanzania yakiwemo madini kusafirishwa kiholela kwenda nje ya nchi.

” Wakati tunashughulika na makinikia walisema hatutofanikiwa na tutashtakiwa lakini leo wote tumeona jinsi ambavyo tumefanikiwa na mabilionea wa Kitanzania akina Laizer wanachimba na kupata madini tena makubwa ambayo yote yanakuza vipato vyao na uchumi wetu.

Magufuli,  Samia Suluhu Hassan, Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally (wa kwanza kulia) na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (wa kwanza kushoto) wakati wa hafla hiyo.

“Ndugu zangu jinsi ambavyo mimi na Makamu wa Rais Mama Samia tulivyopambana kuboresha umeme vijijini ambapo vijiji 9,402 vimepata umeme ilihali wakati tunaingia mwaka 2015 ni vijiji 3,000 tu vilikuwa na umeme tukaona tuna kila sababu ya kuomba tena ridhaa ya kuwatumikia nyinyi watanzania,” amesema Magufuli.

Amesema mafanikio yaliyopatikana nchini ni mengi na wala hayatoshi siku moja pekee huku akisema miaka mitano mingine itakua ni ya kazi zaidi bila kulala lengo likiwa kukuza zaidi uchumi wa Tanzania na kuwasogezea wananchi huduma zaidi.

“Wanasema nitapigiwa kura na Ndege, Madaraja na Vituo vya Afya, mimi nasema asante sana maana wananipigia kampeni, tumenunua ndege 11 tena kwa hela zetu cash hatujakopa na leo tunaona matunda yake, tumejenga flyover ambazo tulizoea kuziona kwenye runinga sasa zipo kwetu na tunazitumia.

Treni za umeme siyo ndoto tena ujenzi wa Reli ya Kisasa unakaribia kukamilika ili treni hizo zipite, ndugu zangu kwa hayo yote nikasema mtu pekee wa kumalizia kazi iliyobaki ni mimi na Mama Samia na chama chetu cha Mapinduzi, ” amesema.

Aidha  amewataka wanachama wa chama hicho kutobweteka kujiona tayari CCM imeshashinda badala yake wazidi kupiga kazi ili kura walizonazo zisipungue.

 Bashiru Ally akimkaribisha  Magufuli  baada ya kuchukua fomu. 

Awali akimkaribisha Dk Magufuli, Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amesema wako tayari kuwakabili wapinzani na kwamba wanaenda kwenye uchaguzi huu wakiwa wenye kujiamini kutokana na mafanikio ambayo yamepatikana kupitia kwake Rais Magufuli na serikali yake.

Spika wa Bunge, Job Ndugai akizungumza katika tukio hilo.

Amesema wao kama viongozi watafanya kampeni za kistarabu na kuwataka wanachama wa CCM kutolala badala yake wapige kampeni za mtaa kwa mtaa, nyumba kwa nyumba na kitanda kwa kitanda.

“Ndugu mgombea wetu utendaji wako mahiri wa kazi ndio unaotupa imani ya kwamba tutaibuka washindi katika uchaguzi huu, jumuiya zetu tumeshazigaia majukumu na zitafanya kazi mchana na usiku kuhakikisha ushindi unapatikana wa kishindo,” amesema Bashiru.

Leave a Comment