×

Sirro: Wanasiasa Fanyeni Siasa za Amani, Utulivu – Video

 

ZIKIWA zimebaki siku chache ili kuanza kwa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2020, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Tanzania, IGP Simon Sirro, amevitaka vyama vya siasa kufanya kampeni za amani na utulivu katika kipindi chote cha uchaguzi na baada ya uchaguzi kwa kile alichodai kuwa kuna maisha baada ya uchaguzi hivyo hawatakiwi kuvunja amani.

 

Sirro amesema hayo leo Jumatano, Agosti 19, 2020, kwenye mkutano uliofanywa jijini Dar es Salaam ukiwakutanisha viongozi wa vyama vya siasa, jeshi la polisi, wadau wa uchaguzi pamoja na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

 

“Uchaguzi utapita salama kama kila mtu ataona umuhimu wa kusimamia amani na utulivu, hakuna sababu ya kusema eshi la polisi linashindana na chama chochote, hatushindani na chama chochote kazi yetu tunayofanya ni tofauti na kazi ya siasa.

 

“Hatushindani na chama chochote, kazi tunayoifanya ni tofauti na ya wanasiasa, na ninawaomba sana wanasiasa watimize wajibu wao. Tusifanye siasa zenye mihemko ambazo zitafanya nchi yetu kuingia kwenye vurugu, vurugu haziwezi kukuingiza madarakani, wananchi wanataka sera na si kejeli na kashifa.

 

“Kuhamasisha watu waingie barabarani matokeo yake ni machafuko, je yakitokea machafuko utamuongoza nani?  Kama unataka kupata uongozi kwa hata kufa, je ukifa utamuongoza nani? Sisi hatuhusiki na usambazaji wa vifaa hivyo lakini vinapocheleweshwa kufika katika vituo husika wananchi huanza kutunyooshea vidole, NEC tunaomba mtusaidie kwenye hili.

 

“Msiingilie kazi ambazo sio zenu, baadhi ya wagombea kutangaza dhana ya kulinda kura ambayo ni kinyume cha sheria, kanuni na taratibu. Tuko vizuri sana kushughulika na wahalifu, mwanasiasa akijiingiza kwenye uhalifu basi huyo ni halali yetu, hakikisheni mnafanya siasa safi za amani na utulivu.

 

“Mungu amewapa vipaji vya kufanya siasa, fanyeni siasa, sisi wengine tumepewa vipaji vya kusimamia amani na utulivu muache tutimize wajibu wetu…kila mtu atimize wajibu wake, na mbaya zaidi ukiingia kwenye wajibu wa mtu mwingine unamchokoza yule anayetimiza wajibu wake,” amesema IGP Simon Sirro.

 

Leave a Comment