×

Sakata la Morrison, Yanga Yatua FIFA – Video

KLABU ya Yanga imesema leo Jumatatu, Agosti 24, 2020, inawasilisha rufaa yake kuhusu sakata la aliyekuwa mchezaji wao, Bernard Morrison,  ambaye hivi karibuni alijiunga na mahasimu wao, yaaniKlabu ya Simba.

 

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Yanga, Dkt. Mshindo Msolla, wakati akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam kuelekea kilele cha Wiki ya Wananchi.

 

“Tupo kwenye ‘Wiki ya Mwananchi’ ambapo uzinduzi wake tumefanya juzi Agosti 22, 2020, Dodoma, shughuli hizi zitaendelea mpaka kwenye kilele ambacho kitakuwa Jumapili, tutacheza na timu ya Aigle Noir ya Burundi.

 

“Wiki ya Mwananchi tumeanza Dodoma, Alhamisi tutakuwa Zanzibar kwa sababu tunataka kufanya kazi katika sehemu zote mbili za Muungano, Jumapili ndipo kilele, na kutakuwa na matukio mbalimbali.

 

“Wachezaji wote wa ndani na wa nje tuliowahitaji tukafanya nao mazungumzo tumeshawasajili. Tumesajili wanane kutoka nje, bado tuna nafasi mbili. Nilisema hizi nafasi mbili na sisi wanachama tuonyeshe kuwajibika, tuchangie tumpe nguvu mdhamini wetu.

 

“Si kwamba wale wachezaji wawili wa Angola wameshindwa kuja hapana, wale tumeshamalizana nao ni issue  (suala) ya tiketi tu muda wowote wanafika, tuna bonasi ya nafasi mbili bado zipo, kama mwaka jana tulichangia wachezaji kumi, mwaka huu hatuwezi kushindwa.

 

“Kuhusu suala la mabadiliko ya klabu tuko vizuri na La Liga na Sevilla, mwisho wa mwezi huu tutapata andiko la kwanza kuhusu tutakavyoendesha klabu yetu, baada ya hapo tutabadilisha katiba ya mwaka 2010 iendane na mahitaji ya sasa ya klabu.

 

“Leo tutafanya submission ya rufaa ya sakata la Bernard Morrison, si kwamba tumenyamaza au tumeliacha, hatujaridhika na maamuzi na leo tunawasilisha rufaa yetu FIFA kule CAS, ili tuone wenzetu wataamua nini.

 

Morrison alikuwa mchezaji wa Yanga kabla ya kujiunga na Simba na kuibua malalamiko yaliyofikishwa katika Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji na kusikilizwa kwa siku tatu, lakini Agosti 12, 2020, Morrison alishinda shauri lake dhidi ya Yanga baada ya kubaini kuwa mkataba wa Yanga unaodaiwa kusainiwa na Morrison ulikuwa na mapungufu.

 

Hata hivyo Klabu ya Yanga ilisema haikuridhishwa na uamuzi uliotolewa na Kamati ya TFF kuwa Bernard Morrison ni mchezaji halali wa Klabu ya Simba, hivyo wakakusudia kukata rufaa katika Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Michezo (CAS) mara watakapopata nakala ya hukumu hiyo.

 

Leave a Comment