CHRISTIANO RONALDO amefikisha magoli 101 tangu aanze kuichezea timu ya taifa ya Ureno baada ya kufunga magoli mawili katika mchezo wa mashindano ya mataifa yaliyopo chini Shirikisho la Soka Barani Ulaya, katika ushindi wa bao 2-0 walioupata kwa Sweden.
Rekodi hiyo inamfanya kuwa mchezaji wa pili kinara wa mabao kwa timu za taifa nyuma ya mchezaji wa zamani wa Iran, Alli Daei, mwenye mabao 109 kutokana na michezo 149 aliyoitumikia taifa lake huku Ronaldo akifikisha magoli hayo 101 katika michezo 165.
Ronaldo alianza kuitumikia timu ya taifa ya Ureno mwaka 2004 katika michuano ya bara la Ulaya maarufu kama (Euro) ambapo Ureno walikuwa wenyeji akiwakuta wachezaji wengi wakubwa na maarufu katika timu hiyo akiwemo Luis Figo, Manuel Rui, Costa Nuno Maniche na wengineo wengi. Alifanikiwa kufunga goli lake la kwanza katika mchezo dhid ya Ugiriki 12/6/2004.
JE RONALDO ANAWEZA KUIPIKU REKODI YA MFUNGAJI BORA WA MUDA WOTE KWA TIMU ZA TAIFA?
Uwezekano ni mkubwa sana licha ya umri wake wa sasa wa miaka 35, anaonekana kuwa bado na nguvu na kwa yale bora aliyoifanyia taifa lake bado ana nafasi kubwa ya kuendelea kuitwa katika kikosi hicho, ambapo anahitajika magoli manane zaidi ili kufikia rekodi za Alli Daei huku akihitajika magoli tisa kuipiku rekodi hiyo ya muda wote ya magoli 109.
Takwimu zinaonyesha kadri umri unavyokwenda mbele zaidi ndiyo kiwango chake kinavyozidi kuimarika, ukiangalia katika magoli yake 101 aliyofunga, magoli 49 ameyafunga akiwa ameshafikisha umri wa miaka 30 huku 52 ameyafunga akiwa na umri chini ya miaka 30; maana yake ni kwamba kadri muda unavyokwenda anabaki kuwa bora.
Ronaldo pia ni mfungaji bora wa muda wote wa Uefa Champions League akiwa na mabao 130 huku mshindani wake wa muda wote ,Lionel Messi, akiwa na mabao 115.
