BERNARD Morrison, kiungo mshambuliaji ndani ya Klabu ya Simba inayonolewa na Kocha Mkuu, Sven Vandenbroeck, ana mechi tatu za moto mkononi ambazo ni sawa na dakika 270 kabla ya kukutana na balaa la Yanga yenye Michael Sarpong mwenye bao moja kwenye ligi.
Morrison kwa sasa amekuwa mfalme mpya ndani ya Simba kwa mujibu wa rekodi akiwa amefunga mabao matatu, pasi moja ya bao na kusababisha penalti moja ndani ya timu hiyo kwenye mechi nne ambazo Simba imecheza mpaka sasa.
Alifunga bao moja mbele ya Vital’O na pasi moja ya bao kwa John Bocco, pia alifunga mbele ya Namungo kwenye fainali ya Ngao ya Jamii na kusababisha penalti moja kwenye ushindi wa mabao 2-0, Uwanja wa Sheikh Amri Abeid.
Kabla ya kukutana na Yanga, Morrison atamalizana na Biashara United, itakuwa Septemba 20, kisha atakutana na Gwambina FC, Septemba 26, zote itakuwa Uwanja Mkapa.
Kete ya mwisho kwa Morrison itakuwa ni Oktoba 10, Uwanja wa Nelson Mandela itakuwa dhidi ya Tanzania Prisons ndipo atakutana na mfalme mpya wa Yanga, Michael Sarpong, Oktoba 18.
Sarpong yeye amehusika kwenye mabao matatu ndani ya Yanga kati ya manne yaliyofungwa kwenye mechi tatu ambazo wamecheza mpaka sasa.
Amefunga mabao mawili na kusababisha kona moja kwenye mchezo wa ligi dhidi ya Mbeya City iliyopigwa na Carlos Carlinhos, ilifungwa na Lamine Moro wakati Yanga ikishinda bao 1-0.
Bao lake la kwanza alilofunga akiwa Yanga, ilikuwa mbele ya Aigle Noir, Uwanja wa Mkapa kwenye mchezo wa kimataifa wa kirafiki na bao la pili aliwafunga Tanzania Prisons ilikuwa kwenye mchezo wa ligi.
Stori: Lunyamadzo mlyuka na manjiro Lyimo, Dar

