POLISI katika Jimbo la Bauchi nchini Nigeria imemkamata mwanaume mwenye umri wa miaka 50 kwa madai ya kumzika mjukuu wake wa kiume mchanga akiwa bado hai.
Msemaji wa polisi ya jimbo la Bauchi, DSP Ahmed Mohammed Wakil, ameiambia BBC kwamba mwanaume huyo aliyetambuliwa kwa jina la Bawada Audu alitekeleza mauaji hayo baada ya binti yake mwenye umri wa miaka 17 kujifungua mtoto wa kiume.
Polisi wanasema msichana huyo alibakwa mwezi Januari, akapata ujauzito na kujifungua na polisi wanasema baba yake msichana alimuua mtoto huyo mchanga.
Wanasema wamepokea taarifa kutoka kwa shirika la kutetea haki za binadamu ambalo halijulikani na walianza kumsaka mshukiwa tarehe 16, Setemba 2020.
“Baba yake msichana alisema kuwa alimpokea mtoto asubuhi baada ya binti yake kujifungua, akaenda nyuma ya nyumba akamzika akiwa bado yu hai,” polisi ya Bauchi ilisema.
Mwanaume huyo pia aliiambia polisi kuwa sababu ya kumuua mjukuu wake ilikuwa ni kwa sababu binti yake alimletea aibu.
Polisi pia wamesema kuwa baada ya kufahamu kuwa mtoto huyo mchanga alizikwa akiwa hai, walikwenda kumfukua alikozikwa na kumpeleka hospitalini, lakini walipofika madaktari walithibitisha kuwa mtoto huyo amekufa baada ya kufanyiwa uchunguzi.
Msichana aliyejifungua mtoto huyo aliiambia polisi kuwa alipewa mimba na mwanamme anayefahamika kama Danjuma Malam Uba, ambaye baadaye alitoroka. Kumekuwa na maandamano na ghadhabu nchini Nigeria miezi ya hivi karibuni kutokana na ongezeko la vitendo vya ubakaji.
Kamanda huyo amesema kuwa uchunguzi unaendelea ili kumsaka mtuhumiwa kwa ajili ya kujibu madai ya kumbaka msichana huyo.
Tatizo la ubakaji linaripotiwa kuwa kubwa katika baadhi ya maeneo nchini Nigeria kiasi kwamba baadhi wametoa wito wa kutolewa kwa adhabu kali dhidi ya wahusika wa ubakaji. Hivi karibuni serikali ya Kaduna iliidhinisha sheria ya kuwahasi wanaume wanaowabaka watoto walio chini ya umri wa miaka 14.
