FAMILIA ya mwanamuziki maarufu duniani kutoka nchini Marekani, John Legend (41) wamepata pigo baada ya kumpoteza mtoto wao waliyemtegemea kumpata ambaye tayari walikuwa wamempa jina la Jack.
Kupitia kwenye Instagram ya mke wa John Legend, Chrissy Teigen (34) ameandika ujumbe mzito kuhusu kutokea kwa jambo hilo ambapo amesema kilichosababisha mtoto wao kufariki ni baada ya kuvuja damu nyingi lakini haijaelezwa kama amefariki akiwa tumboni ama baada ya kujifungua.
Tangu mwanzo wa ujauzito wake, Teigen amekuwa akielezea hali yake ya ujauzito kwenye social media. Mwezi uliyopita alielezea namna alivyokuwa akihangaika na ujauzito wake huo ambao aliupata kwa njia ya kawaida tofauti na ujauzito wa watoto wake wakubwa wawili (Luna miaka 4 na Miles miaka 2) ambao aliupata kwa njia ya kupandikiza (in vitro fertilization – IVF, mnamo Aprili 2016 na May 2018).
Alieleza pia kuwa alikuwa akisumbuliwa na kichwa, kulegea kwa mishipa ya damu hali ambayo ilikuwa inamfanya kukosa nguvu mara kwa mara. Pia mishipa ya ukuta wa mimba ilikuwa imelegea, hali iliyosababisha kupasuka sababu ya pressure kubwa na kusababisha damu nyingi kuvuja.
Hata hivyo amewashukuru wote ambao wamekuwa naye pamoja katika kipindi hiki kigumu akiwemo mwanamitindo maarufu duniani, Kim Kardashian, ambaye amekuwa naye pamoja mwanzo mpaka mwisho katika tatizo.



