KOCHA Mkuu wa Simba, Mbelgiji, Sven Vandenbroeck, amewasikia wapinzani wake atakaokutana nao katika hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika na kutamka kuwa wanatakiwa kujiandaa kwa makini katika kuelekea mchezo huo. Simba ambayo inatarajiwa kuiwakilisha nchi katika Ligi ya Mabingwa Afrika, itapambana na Plateau FC ya Nigeria.
Mechi ya kwanza ni ugenini kati ya Novemba 27- 29, kisha marudiano ni hapa nchini kati ya Desemba 4-6, mwaka huu. Akizungumza na Spoti Xtra, Sven alisema kuwa amepata video za mechi za michezo ya nyuma ambayo wamecheza wapinzani wao Plateau na kubaini kwamba ni timu nzuri inayohitaji uangalizi mkubwa katika kuwakabili.
Sven alisema kuwa wapinzani wao wana timu nzuri yenye washambuliaji wenye nguvu na kasi wakiwa na mpira huku akipanga kuiboresha zaidi safu yake ya ulinzi inayoongozwa na Muivory Coast, Pascal Wawa na Joash Onyango raia wa Kenya.
Aliongeza kuwa pia safu yao ya ulinzi ipo imara, hivyo amepanga kuwaongezea mbinu washambuliaji wake ili kuhakikisha wanapenya kwenye ngome ya Plateau.
“Tunahitaji kujiandaa kwa makini na Ligi ya Mabingwa Afrika. Plateau ni timu ngumu yenye washambuliaji wenye kasi na mabeki imara “Hivyo ili tuweze kuwaondoa na kusonga mbele ni lazima tufanye maandalizi ya kutosha kwa kuboresha kila sehemu ya timu kwa kuanzia mabeki, viungo na washambuliaji ambao nilibahatika kuwaona kwa kupitia video za mechi zao za nyuma walizozicheza,” alisema Sven.
CAF YAIBEBA SIMBA
KATIKA hatua nyingine, Shirikisho la Soka Afrika (Caf), limeongeza idadi ya wachezaji katika vikosi vya timu zitakazoshiriki Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho Afrika msimu huu, hali ambayo itazibeba timu nyingi ikiwemo Simba. Kwa mujibu wa tarifa ambayo imetolewa na Caf, timu zote zishiriki za michuano hiyo ya ngazi ya klabu msimu huu, zimeruhusiwa kuongeza idadi ya wachezaji kutoka 30 na kufi kia 40.
Lengo la kuongeza idadi hiyo ya wachezaji ni kuwepo mchezaji atakayechukua nafasi pale inapotokea kuna kesi ya mchezaji mwenye COVID-19. Pia Caf imeongeza idadi ya wachezaji wa kufanyiwa mabadiliko na kufi kia watano katika mchezo. Wawakilishi wa Tanzania kwenye michuano ya kimataifa ni Simba watakaoshiriki Ligi ya Mabingwa Afrika na Namungo itashiriki Kombe la Shirikisho Afrika.
WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam
