
KIUNGO mkabaji wa zamani wa timu ya taifa ya Senegal, Papa Bouba Diop, 42, amefariki dunia jana Novemba 29, 2020, jijini Paris nchini Ufaransa, baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Bado vyanzo vingi vya habari havijaweka wazi sababu za kifo chake lakini inaripotiwa alikuwa akiumwa kwa muda mrefu.
Papa Diop alipata umaarufu mwaka 2002 katika fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika Korea na Japan baada ya kufunga goli na kuipa ushindi 1-0 wa Senegal dhidi ya Ufaransa ambao ndio walikuwa mabingwa watetezi.

Kwenye fainali hizo Senegal walifika hatua ya robo fainali huku Diop akifunga magoli mawili katika sare ya 3-3 dhidi ya Uruguay.
Papa Diop amewahi kucheza vilabu mbalimbali England kama Fulham, Portsmouth, West Ham United na Birmingham City, Diop alistaafu timu ya taifa 2008 na soka la kimataifa mwaka 2013.