The House of Favourite Newspapers

Namungo Yafafanua Kichuya Kuendelea Kucheza

0

 

KLABU ya Namungo FC ya mkoani Lindi  imetoa ufafanuzi baada ya wadau wengi kuonekana wakihoji kuhusu klabu hiyo kumtumia mchezaji Shiza Kichuya ambaye siku za karibuni zilitoka taarifa kutoka shirikisho la soka duniani (Fifa) kwamba klabu ya Simba imepigwa faini kwa kumtumia mchezaji huyo kinyume na taratibu za usajili.

 

Zilikuwepo pia taarifa kwamba, Kichuya amefungiwa kucheza kwa miezi sita kutokana na sakata lake la usajili kutoka Pharco kwenda Simba.

 

Afisa habari wa Namungo FC Kindamba Namlia amesema: “Kichuya ataendelea kutumiwa na klabu yake kwa sababu klabu ya Simba imeomba FIFA kufanya mapitio upya ya shauri linalomhusu Kichuya.

 

“Katika taarifa tuliyopewa kuhusu Kichuya inasema, Kichuya anaweza kufungiwa miezi sita endapo klabu ya Simba itashindwa kulipa faini ndani ya siku 45.

 

“Mshtakiwa namba moja kwenye shauri lile, Shiza Kichuya, anaweza kufungiwa miezi sita, mshtakiwa namba mbili Simba SC inaweza kufungiwa kusajili kwa misimu mitatu (madirisha matatu makubwa ya usajili).

 

“Kwa sasa Simba imeomba mapitio ya hukumu iliyotolewa na FIFA, kwa maana hiyo kila kitu kinaanza upya hadi mapitio yatakapokamilika. Maana yake hata ule muda iliopewa Simba kulipa faini hauangaliwi hadi pale mapitio yatakapokamilika.

 

“Taarifa itakayotoka baada ya mapitio ndiyo itafanya kazi! Sisi tunajitahidi kwenda kiweledi, baada ya kuipata taarifa kuhusu Kichuya, mtu wetu wa sheria hakuwepo kwa hiyo tulisubiri hadi asome nyaraka za taarifa tuliyopewa kuhusu Kichuya na atupe tafsiri yake.”

Leave A Reply