
KIONGOZI wa kanisa katoliki duniani, Papa Francis, amemchagua mwanamke wa kwanza kuwa katibu katika baraza la mkutano wa maaskofu.
Nathaniel Becquart , ambaye anatoka Ufaransa atakuwa na haki za kupiga kura katika baraza hilo ambalo hutoa ushauri kwa papa na kushiriki katika mijadala inayohusisha masuala tata katika kanisa hilo.
Bi Becquart amefanya kazi katika baraza la mikutano hiyo kama mshauri tangu 2019. Katibu mkuu wa bodi hiyo, Kadinali Mario Grech, alisema kwamba uteuzi huo umeonyesha kwamba ‘mlango umefunguliwa’.
Amesema kwamba uamuzi huo unaonyesha lengo la Papa la kutaka wanawake wengi zaidi kushiriki mchakato wa utambuzi na maamuzi katika kanisa hilo.
Habari hii inakuja chini ya mwezi mmoja baada ya Papa Francis kubadilisha sheria katika kanisa kuwaruhusu wanawake kuhudumu katika madhabahu ingawa amri hiyo ilisisitiza kwamba ukuhani utabaki wazi kwa wanaume pekee.
Mwaka jana, wakati huohuo, Papa huyo aliwateua wanawake sita kwa baraza linalosimamia fedha za Vatican. Mwandishi wa BBC, John McManus, anasema kwamba hatua hiyo siyo sababu ya kuwafanya wanawake kuwa makuhani, japokuwa wanaopinga wanasema kwamba ni hatua inayoelekea upande huo.
Luis Marin de San Martin, ambaye ni kuhani kutoka Hispania, pia aliteuliwa kuwa katibu katika baraza hilo linalompatia ushauri Papa. Katika miaka ya hivi karibuni Sinodi ya Maaskofu imejadili mada za mafundisho ikiwemo jinsi ya kuwashughulikia Wakatoliki waliotalikiana mbali na wale walioolewa.