
MBUNGE wa Temeke Dorothy Kilave ameiomba serikali kuisaidia wilaya hiyo kulipa deni la Sh 12.1 bilioni wanalodaiwa na benki ya CRDB.
Kilave amesema fedha hizo walikopa kwa ajili ya kuwafidia wananchi waliohamishwa katika maeneo yalikotekelezwa miradi ya DMDP. Amesema Sh 19 bilioni zilikopwa na wanalazimika kulipa Sh 4.8 kila mwaka kutoka katika makusanyo ya ndani.
“Mheshimiwa Rais deni hili limekuwa kubwa na zimebaki Sh 12.1 bilioni tunaomba tusaidiwe na serikali ili hizi fedha tunazolipa kila mwaka tuzielekeze kwenye miradi ya maendeleo,” Kilave pia ameomba serikali kuwezesha wilaya hiyo kumiliki eneo lililopo Temeke Mwisho ambalo kwa sasa lipo chini ya TBA.
“Mheshimiwa Rais Temeke tunazaliana sana, kwa siku wanazaliwa watoto kati ya 90 hadi 120 changamoto inakuwa kwenye kuwatunza, vyanzo vya uchumi ni vichache. Tunaomba tupewe lile eneo tufanye uwekezaji ili tuweze kuingiza fedha na kuzalisha ajira,” amesema Kilave