
Familia zimetakiwa kujenga mazoea ya kufanya mazoezi ili Watoto waweze kuelewa umuhimu wa kufanya mazoezi wangali wadogo.
Rai hiyo imetolewa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima wakati alipoungana na wakazi wa Mkoa huu kufanya mazoezi ikiwa ni utaratibu wa Mikoa yote kila jumamosi ili kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza nchini.
Dkt.Gwajima amesema kuwa Baba na Mama wakiwa na mazoea ya kufanya mazoezi kila mara, itawahamasisha Watoto wao kuiga na hivyo kusaidia na kuepusha magonjwa ya kuambukiza ambayo hivi Sasa yanakuja kwa kasi na kuathiri watu wengi nchini na duniani.

“Wazazi mkizoea kufanya mazoezi mtawarithisha watoto angali wadogo na hivyo itasaidia kujikinga na magonjwa kama ya kisukari, moyo, shinikizo la damu na hata uzito uliopitiliza na hivyo kuokoa fedha nyingi kwa ajili ya matibabu na fedha hizo kuelekezwa kwenye kuleta maendeleo katika familia na Taifa kwa ujumla” Alisisitiza Dkt.Gwajima.
Hata hivyo Waziri huyo aliwataka Waganga Wakuu wa Mikoa kuwaelimisha wananchi madhara ya uzito uliopitiliza (unene) na kuwa waweke utaratibu wa kuwapima wananchi uzito kulingana na urefu wao na kutoa ushauri kwa wale watakaokuwa na uzito mkubwa waweze kuanza programu ya kupunguza ili wasipate magonjwa yasiyoambukiza.

Kwa upande wa Lishe, Dkt. Gwajima aliitaka mikoa yote kuwa na Kamati na kuandaa miongozo ya mazoezi kulingana na umri pia maofisa Lishe kutengeneza ‘menu’ inayostahili kulingana na mikoa yao ili Wananchi wanapofanya mazoezi wajue aina za milo wanayopaswa kula.
“Unapofanya mazoezi na kula lishe bora unajiongezea kinga ya mwili na katika lishe epukeni kutumia chumvi na sukari nyingi na kunyweni maji ya kutosha na kupata muda wa kupumzika. Utaratibu huu utawezesha mwili wako uweze kujenga silaha bora zaidi ya kujikinga na magonjwa yasiambukiza ikiwemo changamoto ya upumuaji” Aliongeza.

Waziri huyo pia aliwasisitiza wakazi wa Mkoa wa Katavi kuhusu matumizi ya tiba asili katika kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza na yanayoambukiza kwani miti, mimea na majani yote ni Baraka za Mungu katika nchi yetu.
Dkt.Gwajima hakusita kuwahamasisha Waganga wote wa Tiba Asili/Mbadala kujisajili wenyewe, watoa huduma wao pamoja na bidhaa zao kwenye Baraza la Tiba Asili/Mbadala lililopo chini ya Wizara yake ili kuweka rekodi kwenye Baraza hilo na mamlaka nyingine za Wizara yake.
Na.Catherine Sungura, Katavi