The House of Favourite Newspapers

Polisi Tanzania Yasimamisha Watano

0

UONGOZI wa timu ya Polisi Tanzania, umetangaza kuwasimamisha wachezaji watano kutokana na makosa ya utovu wa nidhamu.

 

Taarifa rasmi kutoka kwa uongozi wa timu hiyo, imebainisha wazi kwamba, nyota hao wamesimamishwa kutokana na tabia hiyo kuota mizizi licha ya kupelekwa mara kadhaa kwenye kamati ya nidhamu.

 

Nyota waliosimamishwa ni Pius Buswita, Rashid Juma, Abdulaziz Makame, Tariq Seif, George Mpole na Abdulmalick Adam.

 

Taarifa hiyo iliyotolewa jana Jumamosi na Ofisa Habari na Mawasiliano wa Polisi Tanzania, Hassan Juma, ilifafanua zaidi kwa kusema Rashid amesimamishwa kutokana na kutofika kambini tangu Februari 29 alipotakiwa arudi baada ya kuomba ruhusa ya kuhudhuria harusi ya kaka yake, huku Mpole akitoroka kambini wakati kikosi hicho kilipoenda Mwanza kucheza na Gwambina FC.

 

Wakati huohuo, kikosi cha wachezaji 20 na viongozi sita wa benchi la ufundi la timu hiyo, wataondoka keshokutwa Jumanne kuelekea Mara tayari kwa mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya wenyeji wao, Biashara United utakaochezwa Aprili 9, mwaka huu, Uwanja wa Karume, Musoma mkoani humo.

STORI NA SAID ALLY | SPOTI XTRA

Leave A Reply