
NI vita ya wababe wa mtaani! Ndivyo unavyoweza kusema baada ya rapa mbabe Bongo, Emmanuel Elibariki almaarufu Nay Wa Mitego ambaye ni C.E.O wa Lebo ya Free Nation na mbabe wa Bongo Fleva, Rajab Abdul au Harmonize ambaye ni C.E.O WA Lebo ya Konde Gang Music Worldwide, IJUMAA linaripoti kamili.
Hata hivyo, katika vita hiyo, mapema tu, asubuhi tu, tayari kimeumana kitaani na Nay au True Boy amewaburuza ‘watoto’ wa Bongo Fleva na kukaa kileleni huku akilia kuchezewa rafu kutokana na umwamba aliouonesha.
NAY ACHUKUA UFALME WA HARMO
Awali, Harmonize au Harmo ndiye aliyekuwa ameshikilia ufalme wa mtaani na wimbo wake wa Teacher, lakini ghafla tu, Nay akaibuka na Wimbo wa Rais wa Kitaa na kumuondoa Konde Boy Mjeshi kwenye midomo ya ‘wana’ huko mitaani.
Kabla ya Wimbo wa Rais wa Kitaa, Wimbo wa Teacher wa Harmonize ndiyo ulikuwa unakamata namba moja ukifuatiwa na Jipinde wa Ibraah ambaye ni msanii aliye chini ya Konde Boy; wote wakitokea Lebo ya Konde Gang.
NANI MJESHI KAMILI?
Saa kadhaa tu, baada ya Nay kuachia Wimbo wa Rais wa Kitaa, akamtupa Harmonize nyuma yake na kukamata namba moja hivyo kuibua gumzo kubwa mtaani kwamba mwenye mitaa yake amerejea hewani na sasa ni tambo tu kwa mashabiki wao; kila mmoja anadai msanii wake ndiye Mjeshi Kamili.
Wakati Wimbo wa Rais wa Kitaa wa Nay ukishika namba moja, ulikuwa hata haujafikisha watazamaji laki 7 (700,000) kwenye Mtandao wa YouTube ilihali Teacher wenyewe ulikuwa na watazamaji zaidi ya milioni 2.4 kwenye Mtandao wa YouTube.
Kwa mujibu wa wataalam wetu wa IT, kuna namna nyingi inaangaliwa ili wimbo uweze kutrendi namba moja ikiwemo watu waliopenda (likes), watu walioutazama (viewers) kwa muda mrefu na pia idadi ya walioweka maoni yao (comments).
Kwa maana hiyo, inavyoonekana kwa harakaharaka, huwenda Nay akawa amebebwa na mashairi ya wimbo wake ambayo yameongelea mambo mbalimbali yanayoendelea nchini ikiwemo suala zima la tozo za miamala ambalo siku za karibuni liliibua mjadala.
Wimbo huo wa Rais wa Kitaa umejaa nondo za kuikosoa Serikali wengine kwa mambo ya tozo, bei ya sukari na sakata la wabunge 19 wa Chadema.
SERIKALI YASHUSHA TOZO
Hata hivyo, Serikali imeshusha tozo hizo za miamala siku moja tu baada ya Nay kuachia wimbo huo wa Rais wa Kitaa.
Wimbo huo ulipotoka tu, baadhi ya watu walidai Nay atakutana na yaleyale aliyozoea kukutana nayo; yaani nyimbo zake za kiharakati kufungiwa na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata), lakini hadi jana, Alhamisi, Septemba 2, 2021, hakuna jambo kama hilo.
RAIS WA KITAA YASHIKISHA ADABU
Wimbo wake huo wa Nay mwenye wafuasi (subscribers) takriban laki 3 tu, umeweza kuzishinda nyimbo kama Teacher wa Harmo mwenye wafuasi (subscribers) milioni 2.75, Happy Birthday wa Rayvanny mwenye wafuasi (subscribers) milioni 3.13 na wasanii wengine kibao ambao nyimbo zao zimeshika adabu kwa Rais wa Kitaa.
NAY ALIA KUCHEZEWA RAFU
Katika mazingira kama hayo, Nay amejikuta akilia kuchezewa rafu na kuomba msaada kwa mashabiki wake kufuatia
kushuka kwa views (watazamaji) wa wimbo huo kutoka laki 587,000 hadi 552,000.
Nay amesema; “Wataalam hebu nisaidieni shida inakuaga nini views kushuka.?! Ilikuwa 587K imeshuka mpaka 552K. Shida ni nini tenaaa.?! ”Hata hivyo, baadaye views ziliendelea kupanda kama kawaida.
NAY: WANAONISAPOTI KULA YAO NI SHIDA
Akizungumza na Gazeti la IJUMAA juu ya wimbo huo, Nay anasema kuwa, yeye ni kioo cha jamii na anawakilisha mawazo na shida walizonazo mashabiki wake wengi mtaani.
“Wanaonisapoti kula yao ni shida, lakini wananipenda, mashabiki wangu wengi asilimia kubwa ni walalahoi, watafutaji, wamachinga na wengi wenye maisha ya kuungaunga na wananisapoti hivyo nahitaji kuwasapoti kwa kuwa upande wao,” anasema Nay wa Mitego.
NYIMBO ZILIZOMPONZA NAY
Baadhi ya nyimbo za Nay ambazo zimewahi kuzua utata mkali, kumuingiza kwenye matatizo na wakati mwingine kufungiwa na Basata ni pamoja na Shika Adamu Yako, Mama, Pale Kati Patamu na sasa Rais wa Kitaa na nyinginezo.
STORI; KHADIJA BAKARI, DAR