The House of Favourite Newspapers

Ninja Awatangazia Vita Wanigeria

0

BEKI wa kati wa Yanga, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ amewachimba mkwara wapinzani wao katika Ligi ya Mabingwa Afrika, Rivers United kutoka Nigeria kuwa wasitarajie kupata matokeo yenye faida katika mchezo wanaokwenda kucheza kwa kuwa wamejipanga kufanya makubwa.

 

Ninja ametoa kauli hiyo kabla ya mchezo huo wa hatua ya awali unaotarajia kupigwa leo Jumapili kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar, kisha kurudiana Jumapili ijayo nchini Nigeria.

Akizungumza na Spoti Xtra, Ninja alisema kuwa ukubwa wa kikosi chao pamoja na kuwepo kwa wachezaji wengi wenye uzoefu utawasaidia kupata matokeo mazuri kwenye mchezo wao wa kwanza wa hatua ya awali kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

“Nadhani kikubwa kwetu ni ushindi kutokana na hali ya wachezaji kutokana na maandalizi ambayo klabu yetu ambayo tunafanya kwa ajili ya mchezo wa Jumapili, kikubwa tunahitaji kupata matokeo makubwa ambayo yatakuwa msaada kwenye mechi ya marudiano.

 

“Unajua hatuwezi kuamini kama wapinzani wetu ni bora au siyo bora, tunawaheshimu kutokana na kuwepo kwao katika michuano hii, lakini bado uzoefu wa wachezaji ambao tupo kwa sasa katika michuano ya kimataifa, naamini itatubeba kupata ushindi kwa sababu ndiyo malengo yetu,” alisema Ninja.

Leave A Reply