×

Mayele: Kazi Imeanza, Nitafunga Sana

STRAIKA Mkongomani, Fiston Mayele, ametoa kauli ya furaha kwa mashabiki wa Yanga akisema bao alilofunga dhidi ya Simba ni mwanzo tu, furaha kubwa inakuja msimu huu wa 2021/22.

 

Kauli hiyo aliitoa muda mchache baada ya mchezo wa Ngao ya Jamii uliopigwa Uwanja wa Mkapa, Dar, ambao ulimalizika kwa Yanga kushinda bao 1-0 na kunyakua Ngao ya Jamii, huku yeye akifunga bao hilo pekee dakika ya 12.

 

Akizungumza na Spoti Xtra, Mayele alisema ana furaha kubwa kufunga bao katika dabi yake ya kwanza aliyoicheza msimu huu, huku akiahidi kuendelea kufunga katika Ligi Kuu Bara na mashindano mengine.

 

“Kuwafunga Simba siyo kama nimebahatisha, nimezoea kufanya hivyo kwenye dabi kwani nyumbani nikiwa na AS Vita nilishacheza dabi ambayo ni ngumu na yenye ushindani kama hii ya Simba dhidi ya Yanga.

 

“Kikubwa ninafurahia kufunga bao langu la kwanza la mashindano nikiwa na Yanga, ambalo limetupa Ngao ya Jamii.

 

“Niwaahidi mashabiki wa Yanga kwa kuwaambia kuwa furaha kubwa inakuja ligi ikianza, ninafahamu ligi ni ngumu lakini nitapambana kuhakikisha tunachukua ubingwa,” alisema Mayele na kuongeza kuwa.

 

“Malengo yangu katika msimu huu ni kuhakikisha napambana ili kuwa mfungaji bora wa ligi na kuipatia timu yangu ubingwa, najua kila mchezaji ana malengo yake, lakini kwa upande wangu nitahakikisha ninapambania malengo yangu kwa bidii.

 

“Najua sio jambo rahisi, lakini biidi zaidi na kujituma ndio kitu pekee kitakachonifikisha pale ninapotaka, kama unavojua Ligi ya Tanzania ni ngumu sana na ina ushindani wa hali ya juu unayoifanya iwe bora kila siku zinavozidi kwenda, hivyo hata mimi nimejiandaa kwenda sawa na ubora wake.”

 

Msimu uliopita, Tuzo ya Mfungaji Bora ilikwenda kwa John Bocco wa Simba aliyefunga mabao 16. Ukitazama sasa hivi kikosi chao unaona kimeimarika katika kila idara jambo ambalo linampa mwalimu wakati mzuri wa kufanya chaguzi kwenye kikosi chake.

~~WILBERT MOLANDI NA HAWA ABOUBAKHARI, Dar

Leave a Comment