The House of Favourite Newspapers

Mastaa Simba SC Wawekewa Milioni 300

0

KATIKA kuhakikisha wapinzani wa Simba, Jwaneng Galaxy wanapotea vibaya wakiwa kwao, uongozi wa Klabu ya Simba umeweka mezani shilingi milioni 300 ambazo zitakuwa zawadi kwa wachezaji endapo watafanikiwa kuibuka na ushindi.

Oktoba 17, mwaka huu, Simba itakuwa na kibarua kizito cha kupambana na Jwaneng Galaxy katika mchezo wa hatua ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika utakaofanyika nchini Botswana.

Chanzo cha ndani kutoka Simba, kimeliambia Spoti Xtra kuwa, kama kawaida ya uongozi wa klabu hiyo chini ya mwekezaji wake, Mohammed Dewji, walikuwa wakitoa fedha za motisha kwa ajili ya kusaka ushindi, hivyo kuelekea katika mchezo dhidi ya Jwaneng tayari kiasi kilekile ambacho kilikuwa kikitolewa msimu uliopita tayari kimetengwa.

“Tayari shilingi milioni 300 ambazo zilikuwa zikiwekwa msimu uliopita katika michezo ya Ligi ya Mabingwa Afrika, zimewekwa tena msimu huu katika mchezo wa kwanza ambao Simba itacheza dhidi ya Jwaneng Galaxy.

“Nia ya kuwekwa kwa motisha hiyo kwanza uongozi wa Simba unahitaji timu kufanya vema katika michuano hiyo kwa kuhakikisha haitoki hatua za awali kama ilivyotekea msimu wa 2019/2020 ambapo tulitolewa na UD Songo,” kilisema chanzo.

Alipotafutwa Mwenyekiti wa Simba, Murtaza Mangungu kuhusiana na kuwekwa kwa mzigo huo, alisema: “Uongozi wa timu hutoa fedha za motisha katika michuano hii ya kimataifa, lakini huwa tunafanya siri kwa ajili ya maslahi ya wachezaji.”

 

r MARCO MZUMBE, Dar es Salaam

Leave A Reply