
SERIKALI ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimesema zitaendelea kushirikiana kwa ukaribu na kampuni ya mawasiliano ya simu za mkononi Zantel ambayo kwasasa imeungana na mtandao wa tigo, katika kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za mawasiliano kwa wananchi wake.
Hayo yamebainishwa kwa nyakati tofauti visiwani Zanzibar, na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye mara baada ya kufanya ukaguzi wa shughuli ya ujenzi wa minara ya mawasiliano inayoendelea kujengwa katika maeneo mbalimbali ya visiwa vya Unguja na Pemba.

Nape amesema kuwa hatua hiyo ya ujengwaji wa minara ya mawasiliano inayofanywa na kampuni ya Zantel ambayo kwasasa imeungana na mtandao wa tigo imekuja kufuatia maelekezo ya Raisi wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Hussein Ali Mwinyi ya kutaka kuhakikisha wananchi wote wa visiwa hivyo wanapata huduma bora za mawasiliano popote walipo.
“Sasa tumekuja kuona utekelezaji umefikia kiasi gani ili kama kazi imekamilika tumkabidhi Raisi kwamba maagizo aliyoyatoa yamekamilika kwa kiasi gani,”alisema.
Akielezea hali ya ujenzi inavyoendelea kwasasa Meneja wa Mradi (Project Manager) wa Kampuni ya Zantel Bw. Mohamed Ahemd Jai amesema zoezi la ujenzi wa minara hiyo linaendelea vizuri, sambamba
na kutoa shukrani zake kwa mamlaka husika kwa kurahisisha upatikanaji wa vibali vilivyo wezesha shughuli hiyo kuanza kufanyika.
Aliongeza kwa kusema kuwa anaimani kukamilika kwa zoezi la ujenzi wa minara hiyo kutapelekea kwa asilimia kubwa changamoto ya mawasiliano imetatuliwa hususani maeneo yanayo kabiliwa na matatizo ya mawasiliano.
Mapema akisoma taarifa fupi kuhusu mradi huo Mwakilishi wa Kampuni ya zantel na Tigo mbele ya waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, amsema licha ya kufanikiwa kwa kiasi kikubwa juu ya zoezi hilo lakini pia amabainisha baadhi ya changamoto walizokubana nazo hapo awali ikiwemo kukataa kwa wenye maeneo yao kwa dakika za mwisho kabla kuanza kutekeleza mradi huo.
Ziara ya hiyo ya kukagua zoezi la ujengaji wa minara ya mawasiliano ambapo minara Arobaini na mbili (42) itajengwa Visiwani Zanzibar ni ya siku mbili kwa waziri Nape Nnauye ambapo leo hii ameanzia kukagua kisiwa cha Unguja katika Mkoa wa Kaskazini Unguja na ikisha ataelekea kisiwani Pemba kwa kazi hiyo hiyo.