
Kampuniya Bia ya Serengeti (SBL) imesema itaendelea kuwawezesha vijana ili waweze kuwa na ushiriki mpana zaidi katika kilimo.
Akiongea wakati wa kukabidhi vyeti kwa wanafunzi 27 wanaofadhiliwa na kampuni hiyo chini ya program ya Kilimo Viwanda katika chuo cha Kilimo na Mifugo Kaole, mkurugenzi wa mahusiano kwa umma wa SBL John Wanyancha alisema SBL inatambua umuhimu wa vijana kushiriki katika kilimo

“Vijana ambao tunawafadhili chini ya program ya Kilimo viwanda, watakwenda kuongeza nguvu kwenye sekta hii muhimu kwa uchumi wa nchi yetu. Mchango wao utakuwa muhimu sana katika kuhakikisha kilimo chetu kinakuwa na tija,” alisema.
Wanyancha alisema SBL hutumia malighafi zinazotokana na kilimo kutengenezea bia zake ikiwa ni Pamoja na shayiri, mtama na mahindi na kuongeza kuwa uwepo wa wataalamu wa kutosha utasaidia upatikanaji wa malighafi hizo ambazo mahitaji yamekuwa yakiongezeka

“Mahitaji yetu ya malighafi yanaongezeka kilamwaka. Mwaka 2021 kwamfano tulinunua tani 18 za malighafi ambazo ni sawa na asilimai 80 ya mahitaji yetu kwa mwaka. Lengo letu ni kufikia asilimia 85 ifikapo mwaka 2025,” alieleza
Kupitia program ya kilimo Viwanda, SBL tayari imeshatoa ufadhili kwa wanafunzi zaidiya 200 wanasomea masomo ya kilimo katika vyuo vine ikiwa Pamoja na Kaole cha Bagamoyo, Kilacha cha Moshi Mt. Maria Goretti cha Iringa na Igabiro kilichopo Muleba mkoani Kagera..
Kwa upande wake mkuu wa chuo cha Kaole Sinani Simba aliishukuru SBL kwa kutoa ufadhili kwa wanafunzi ambao amesema pasipo msaada huo wengi wao wangeshindwa kumaliza masomo yao kutokana na changamoto ya kushindwa kulipa ada.
“Mchango wa SBL siyo tuu kuwasaidia wanafunzi wanaotoka katika familia duni kupata fursa ya kuendelea na masomo, bali pia unasaidia kukuza sekta ya kilimo hapa nchini kupitia kuongeza wataalamu ambao takwimu zinaonyesha ni wachache ukilinganisha na mahitaji,” alisema.