×

Naibu Waziri Kilimo, SBL Waongoza Wakazi Dodoma Kupanda Miti, Kuondoa Ukame

Walioketi: Naibu Waziri wa Kilimo Anthony Mavunde (Katikati), Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bia ya Serengeti Mark Ocitti (pembeni kulia), SSP John Nyonyi (Pembeni ya Ocitti) na George Lucas Tadey (mwisho kushoto) Mweka Hazina wa Asasi ya kiraia Habari Development Association (HDA) katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa SBL na wakazi wa eneo la Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili Mirembe wakati wa zoezi la upandaji miti elfu tano uliofanyika asubuhi ya leo.

 

Dodoma, Julai 6, 2022 – Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) kwa mara ya pili, leo imeungana na viongozi pamoja na wananchi wa eneo la hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili Mirembe mkoani Dodoma katika zoezi la upandaji maelfu ya miti ikiwa ni sehemu ya mpango wa kampuni hiyo wa kukabiliana na ukame.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) Mark Ocitti akinawa mikono baada ya kupanda mti katika eneo la Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili Mirembe, jijini Dodoma asubuhi ya leo. Pembeni yake kuilia ni Naibu Waziri wa Kilimo Mark Ocitti anayeuangalia mti aliupanda. Shughuli hiyo imesimamiwa na asasi ya kiraia, Habari Development Association (HDA) ikishirikiana na SBL katika kukabiliana na ukame na kutunza mazingira mkoani Dodoma.

 

 

Katika kuonyesha jitihada za makusudi za kukabiliana na ukame na kutunza mazingira, Naibu Waziri wa Kilimo na Mbunge wa Dodoma mjini Anthony Mavunde, Katibu wa Afya Hospitali ya Taifa ya Akili Mirembe, Jackson Mjinja, viongozi wa jeshi na magereza ni baadhi ya viongozi walioshiriki katika zoezi hilo la upandaji miti lililoandaliwa na SBL kwa kushirikiana na asasi isiyo ya Kiserikali ya Habari Development Association (HDA).

Akiongea wakati wa zoezi hilo, mkurugenzi mtendaji wa SBL Mark Ocitti alisema upandaji miti katika hospitali ya Mirembe ni sehemu ya mkakati endelevu wa kampuni hiyo unaolenga kupanda maelfu ya miti sehemu mbali mbali hapa nchini.

 

Mkurugenzi huyo alisema mwaka 2019 kampuni ya SBL ilipanda miti katika wilaya za Same

Pamoja na Moshi ili kuongeza uotokatika maeneo ya jirani na mlima Kilimanjaro. “Upandaji miti wa SBL hapa unaendeleza jitihada zingine zilizofanya katika mikoa tofauti nchini na kampuni, ikiwemo wilayani Kongwa mwaka jana, ambapo SBL ilipanda maelfu ya miti” alisema Ocitti.

Mkurugenzi Mtendaji wa SBL Mark Ocitti akiumwagilia maji mti alioupanda kulia Waziri Mavunde na wakazi wengine walioshiriki zoezi hilo wakishuhudia.

 

 

Upandaji miti wa SBL unakuja katika kipindi ambacho dunia inahangaika kupunguza uzalishaji ya hewa ukaa ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabia ya nchi pamoja na kuyalinda mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

 

“SBL na kampuni mlezi wake, Diageo, zinachukulia utunzaji wa mazingira kwa umakini mkubwa kama kitovu cha mafanikio ya mchakato wa uzalishaji” aliongeza Ocitti. Kwa upande wake Naibu waziri aliishukuru kampuni ya SBL kwa kuunga mkono jitihada za upandaji miti na kuongeza kuwa miti ina nafasi ya kipikee kwa maisha ya watu na kusistiza kuwa bila miti hakuna maisha.

 

Zaidi ya yote, alisisita kulifanya eneo hilo kuwa kivutio cha utalii cha asili kupitia miti hiyo iliyopandwa. “Leo tunaianza kampeni hii pamoja na wenzetu wa SBL. Ni imani yangu kwamba tutaisimamia, tutaiendeleza, ili lengo letu kuu liweze kutimia” Waziri alisema.

 

Naibu Waziri alisema ukataji miti holela ni moja kati ya sababu za mabadiliko ya tabia ya nchi ambayo yamesababisha changamoto nyingi zinazomkabili binadamu ikiwa ni pamoja na athari kwenye uzalishaji wa chakula, upatikanaji wa maji, mbuga za wanyama na afya ya viumbe mbali mbali ikiwa ni pamoja na binadamu.

 

“Nina amini kuwa zozei hili la upandaji miti litawapa hamasa wakati wa mjini Dodoma na maeneo mengine nchini kupanda miti kila wanapopata fursa. Pia napenda kuzikumbusha taasisi na makampuni mbali mbali kufikiria juu ya dunia yetu na kuchukua hatua za kuilinda na kuitunza,” aliongeza Waziri.

 

Katibu Mkuu Mtendaji wa HDA, Bernard James aliishukuru SBL kwa jitihada zake za makusudi kutunza mazingira na kupambana na ukame nchini na hasa kuitumia taasisi hiyo kuifanya Dodoma kuwa ya kijani.

Leave a Comment