
UONGOZI wa Yanga umeweka wazi kuwa, mastaa 7 wa timu hiyo watajiunga na wenzao kambini mara baada ya kumaliza majukumu ya timu ya taifa Julai 30, mwaka huu.
Kutokana na kuchelewa kwao, Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi, itabidi awasubiri kwa takribani wiki moja ndipo aendelee kushusha madini zaidi katika kukisuka kikosi hicho.
Yanga ambayo jana Jumamosi jioni ilianza mazoezi rasmi kujiandaa na msimu wa 2022/23 wakiweka kambi AVIC Town, Kigamboni, Dar, ilianza bila ya wachezaji hao saba waliopo na kikosi cha Taifa Stars ambacho jana kilicheza mchezo wa kufuzu CHAN 2023 dhidi ya Somalia.
Baada ya mchezo wa jana, Taifa Stars itarudiana na Somalia wikiendi ijayo. Ofisa Habari wa Yanga, Hassan Bumbuli, ameliambia Spoti Xtra, kuwa: “Kambi itakuwa AVIC Town, kumbuka kwamba tuna wachezaji wapo timu ya taifa, wao wataungana na wenzao wakimaliza majukumu ya timu ya taifa.”
Wachezaji wa Yanga ambao wapo ndani ya Taifa Stars ni Aboutwalib Mshery, Kibwana Shomari, Dickson Job, Bakari Mwamnyeto, Feisal Salum, Farid Mussa na Salum Aboubakar.