×

Wizara ya Elimu yakutana na Wahariri, Yaeleza Vipaumbele Vyake

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda akizungumza na Wahariri wa Vyombo vya Habari juu ya Mwelekeo wa Wizara, Vipaumbele na Maeneo ya Kimkakati katika Utekelezaji kwa Mwaka wa Fedha 2022/23 leo tarehe 29 Julai 2022 Jijini Dar es Salaam.
Elimu ujuzi ni miongoni mwa hatua na mikakati muhimu ambayo Serikali inaiendeleza kwa kuwa inatambua licha ya elimu ujuzi kuwa na manufaa pia ni njia rahisi ya kila mtu kuwa na uwezo wa kujiajiri au kuajiriwa.
Ameyasema hayo leo Julai 29,2022 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda wakati akizungumza na Wahariri wa Vyombo vya Habari juu ya Mwelekeo wa Wizara, Vipaumbele na Maeneo ya Kimkakati katika Utekelezaji kwa Mwaka wa Fedha 2022/23 .
Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH). Dkt Amos Nungu akizungumza katika mkutano wa Wizara ya Elimu , Sayansi na Teknolojia pamoja na Wahariri wa Vyombo vya Habari
“Baadae tunatarajia kuona elimu ujuzi inashika nafasi kubwa ili kuhakikisha kila mwanafunzi anatumia ujuzi wake kwa manufaa ya jamii na Taifa kwa ujumla”. Amesema Waziri Mkenda.
Amesema Serikali itaendelea kuhakikisha inatoa elimu katika maeneo yanayofika kwa ajili ya wananfunzi wote na pale ambapo kuna ugumu kuangalia namna ambavyo itajenga shule za mabweni ili kuwapa nafuu wanafunzi.
Aidha amesema Serikali imetenga shilingi Bilioni 3 kwa mwaka huu kwa ajili ya kuwezesha ufadhili kwa wanafunzi ambao wamepata ufaulu mkubwa katika elimu ya juu kupitia masomo ya sayansi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda akipata picha ya pamoja na Wahariri wa Vyombo vya Habari kwenye mkutano ambao Wizara ikielezea juu ya Mwelekeo wa Wizara, Vipaumbele na Maeneo ya Kimkakati katika Utekelezaji kwa Mwaka wa Fedha 2022/23 leo tarehe 29 Julai 2022 Jijini Dar es Salaam.
“Kigezo cha atakayepatiwa ufadhili huo ambao wengi wanataka uitwe Samia Scholar ni kufaulu vizuri katika masomo ya sayansi na upo tayari kuendelea na kusoma masomo ya uhandisi,elimu tiba.Kwa sasa tunatoa udhamini huo kwa vyuo vya ndani tu,”amesema Prof.Mkenda.
Amesema wataweka dirisha kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu ili nao waweze kunufaika na ufadhili huo ambao utakuwa unatolewa bila kujali huyu katoka wapi au familia gani, ilimradi awe amefaulu vizuri sayansi na afahamu kuwa, anasoma kwa kodi ya Watanzania, hivyo anapaswa kuonesha bidii ili aje kuwahudumia kupitia taaluma yake.

Leave a Comment