Ofisi ya DC Jokate Yagawa Vifaa Tiba Kwa Wajawazito 200, Mpango Unaendelea
19 Novemba 2022: Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Jokate Mwegelo imegawa vifaa tiba kwa kinamama wajawazito zaidi ya 200 kwenye hospitali ya Mbagala Rangitatu, jijini Dar huku ikiahidi kuendelea kugawa misaada hiyo.
Akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa Temeke Maternal Jogging, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Jokate Mwegelo aliyejitambulishwa kwa jina la Theodora Mnata amesema mpango huo wa BUSELA upo chini ya Hatua African Group.
Mwakilishi huyo amesema lengo kuu la mpango huo ni kuisapoti serikali katika kuhamasisha jamii ikiwemo wajawazito kufanya mazoezi, kupata lishe bora na kuwajenga kisaikolojia wakati wa ujauzito.
Mwakilishi huyo amesema kumekuwa na changamoto nyingi sana za vifo vya wajawazito wakati wa kujifungua kutokana sababu mbalimbali ikiwemo na ukosefu wa lishe bora, ukosefu wa vifaa tiba wakati wa kujifungua na wakati mwingine matatizo ya kisaikolojia.
Naye Mkurugenzi wa Hatua Group Africa, Derick Mgaya amesema kwenye kampuni hiyo kuna mpango uitwao BUSELA ambao lengo lake kubwa ni kuwasaidia wajawazito katika mpango wa lishe, kufanya mazoezi na kuwajenga kisaikolojia.
Derick amesema mpango huo mpaka sasa umeshawasaidia wajawazito zaidi ya elfu mbili na lengo ifikapo 2023/24 ni kuwafikia kinamama laki tatu.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Deity ambao ni watengenezaji na usambazaji wa vifaa tiba vya wajawazito amesema wameamua kuungana na mpango wa BUSELA kwa ajili ya kuisaidia serikali katika mpango wa kuwasaidia wajawazito katika mpango wa uzazi salama. HABARI/PICHA:RICHARD BUKOS/ GLOBAL PUBLISHERS