The House of Favourite Newspapers

Kigogo wa Jatu PLC Afikishwa Mahakamani Kisutu

0

Kutoka katika Mahakama ya Hakimu mkazi kisutu ni kwamba Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya JATU PLC, Peter Gasaya amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kujibu shtaka moja la kujipatia Sh5.1 bilioni kwa njia ya udanganyifu.
Gasaya anadaiwa kujipatia fedha hizo kutoka katika Saccos ya JATU kwa madai ya kuwa fedha hizo atazipanda kwenye kilimo ili kuzalisha faida zaidi, wakati akijua kuwa ni uongo.
Mshtakiwa huyo amefikishwa mahakamani hapo leo Alhamisi Desemba 29, 2022 na kusomewa shtaka lake na wakili wa Serikali Tumaini Mafuru, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Mary Mrio.
Akisomewa shtaka hilo, wakili Mafuru amedai kuwa mshtakiwa anakabiliwa na kesi ya jinai namba 207/2022 yenye shtaka moja la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.
Wakili amedai kuwa mshtakiwa andaiwa kutenda kosa hilo, kati ya Januari Mosi, 2020 na Desemba 31, 2021 katika Jiji la Dar es Salaam, akiwa kama Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo, kwa njia ya udanganyifu alijipatia Sh 5,139,865,733 kutoka Saccos ya JATU.
Mshtakiwa baada ya kusomewa shtaka lake, amekana kutenda kosa hilo na upande wa mashtaka umedai kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika.
Hakimu Mrio baada ya kusikiliza maelezo ya pande zote, amesema kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kutoa dhamana kwa kesi yenye shtaka linalozidi kiwango cha Sh300 milioni.
Baada ya kueleza hayo, Hakimu Mrio ameahirisha kesi hiyo hadi Januari 11, 2023 itakapotajwa tena.
Leave A Reply