
Rais wa Urusi Vladimir Putin amemuondoa kamanda mkuu wa nchi hiyo aliyekuwa anaongoza vita Ukraine, miezi mitatu tu baada ya kuteuliwa.
Mkuu wa Majenerali Valery Gerasimov sasa ataongoza kile ambacho Bw Putin anaita “operesheni maalum ya kijeshi”.
Jenerali Gerasimov anachukua nafasi ya Sergei Surovikin ambaye amesimamia mashambulizi ya hivi majuzi ya kikatili dhidi ya miundombinu ya nishati ya Ukraine.
Mabadiliko hayo yanakuja huku Warusi wakidai kuwa wanapiga hatua mashariki mwa Ukraine.
Urusi ilianzisha uvamizi wake nchini Ukraine tarehe 24 Februari.
Jenerali Gerasimov, ambaye amekuwa kwenye wadhifa huo tangu 2012, ndiye mkuu wa wafanyakazi wakuu wa Urusi aliyekaa muda mrefu zaidi tangu enzi ya baada ya Soviet.
Jenerali Surovikin – amepewa jina la “Jenerali Armageddon” kutokana na mbinu zake za kikatili katika vita vya awali, ikiwa ni pamoja na operesheni za Urusi nchini Syria na mashambulizi makubwa ya mabomu katika mji wa Aleppo hasa.
Muda mfupi baada ya kuteuliwa kuongoza operesheni hiyo mwezi Oktoba, Urusi ilianza kampeni yake ya kuharibu miundombinu ya nishati ya Ukraine, na kuwaacha mamilioni ya raia wa Ukraine bila umeme au maji ya bomba kwa muda mrefu.
Pia alisimamia kujiondoa kwa Urusi kutoka mji wa kusini wa Kherson – mafanikio makubwa kwa Waukraine.