×

RC Chalamila Atoa Neno Kuelekea Mkutano Jukwaa Mifumo ya Chakula Afrika

WAKATI Tanzania ikijiandaa kupokea ugeni wa viongozi wakuu wa nchi mbalimbali pamoja na wadau wa mifumo ya chakula Afrika kwa ajili ya mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula Afrika(AGRF), Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amewataka wananchi kuchangamkia fursa.
Mkutano huo unatarajia kuanza Septemba 5 hadi Septemba 8 mwaka huu na maandalizi ya kuufanikisha mkutano huo mkubwa yamekamilika na inaelezwa mkutano huo utaleta matokeo chanya katika uendelezwaji wa mifumo ya chakula kwa nchi za Afrika, ukuzaji sekta ya utalii, uwekezaji sekta ya kilimo na biashara.

Akizungumza leo Septemba 1, 2023 na waandishi wa habari kuhusu mkutano huo utakaokuwa na washiriki zaidi ya 3000, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Saaam Albert Chalamila ametumia nafasi hiyo kuwahimiza wananchi kuchangamkia fursa zitazopatikana kupitia jukwaa hilo.
Chalamila amefafanua AGRF ni jukwaa kuu la kilimo pamoja na mambo mengine limekuwa likiweka mipango na mikakati ya kiutendaji sambamba na kuhakikisha wanajadili kwa kina kuhusu usalama wa chakula barani Afrika.

“Wananchi wa Dar es Salaam na maeneo mengine mnapaswa kuchangamkia fursa ambazo zitatokana na kufanyika mkutano huu mkubwa.Kupitia mkutano wa jukwaa hilo pia tutapata fursa za kujifunza teknolojia za kisasa pamoja na na kuongeza uzoefu na hatimaye tutafikia malengo yaliyowekwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere JNICC Ephrahim Mafuru ameeleza Serikali ya Tanzania inatarajia kupokea washiriki zaidi ya 3000 ambao watahudhuria mkutano huo.
Ameongeza kwamba katika kufanikisha mkutano huo Sh.bilioni 12.5 zimetolewa huku akifafanua JNICC wamejipanga vema kuwapokea na kuwahudumia washiriki wote.
Akifafanua zaidi amesema kutokana na ugeni huo vyumba zaid ya 2600 vya hoteli tayari vimeandaliwa.” Nitoe rai wananchi tuchangamkie fursa na wale ambao watapata nafasi ya kushiriki haswa wajasiriamali jukwaa hili ni sehemu nzuri ya kukutana na wadau kubadilishana uzoefu.”

Leave a Comment