×

Serikali ya Rais Samia Yatekeleza Miradi 11 Katika Jiji la Dar es Salaam

Katika kipindi cha miaka mitatu, serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imetekeleza zaidi ya miradi 11 katika Jiji la Dar es Salaam kati ya hiyo mradi 8 ni mikubwa ya kimkakati na 3 ni midogo ambayo itasaidia kutatua changamoto za barabara kutopitika vizuri na kupunguza msongamano wa magari.

Akizungumza na waandishi wa habari Machi 11, 2024 kuhusu mafanikio ya serikali ya awamu ya sita katika sekta ya ujenzi wa miundombinu ya barabara na madaraja; Meneja wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Dar- es Salaam Mhandisi John Mkumbo amesema kati ya miradi hiyo, mitano imekamilika na 6 inaendelea kutekelezwa.

Amesema miongoni mwa miradi ya maendeleo inayotekelezwa ni pamoja na mabasi ya mwendo wa haraka awamu ya pili (BRT 2) katika barabara ya Da- es Salaam – Kongowe eneo la Mbagala Rangi tatu, Chang’ombe (Keko- Mgulani JKT), Kawawa (Veta Chang’ombe JCT- Magomeni Mapipa) na Sokoine ambapo mradi umefikia 98%.

Amesema ujenzi wa miundombinu ya mabasi yaendayo haraka awamu ya tatu (BRT 3) km 23 katika Barabara ya Tanganyika Motors – DIA TI, Uhuru (Buguruni – Msimbazi ) Bibi titi na Shauri moyo ( Karume – Bohari), unaendelea pamoja na ujenzi wa miundombinu ya mabasi yaendayo haraka awamu ya nne (BRT 4) unaoanzia maktaba ya Taifa – Mwenge – Sam Nujoma km 13.5 ambao unapita pia katika barabara ya Mwenge – hadi (DAWASA) Tegeta km 15.63.

Pia kuna utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa barabara ya Morogoro kutoka njia mbili kwenda njia nane km 19 na maegesho ya magari Kiluvya yenye urefu wa mita za mraba 36,000 awamu ya kwanza ikihusisha ujenzi wa maegesho yenye ukubwa wa mita za mraba 18,000 yatakayokuwa na uwezo wa kuchukua wastani wa malori zaidi ya 200 kwa siku, lengo ni kuondoa maegesho yasiyo rasmi pembezoni mwa barabara ya mandela na hivyo kupunguza foleni zinazoweza kuepukika.

Leave a Comment