×

Video: ‘House Girl’ Afikishwa Mahakamani Kwa Tuhuma Za Kujaribu Kuua Kichanga

Faima Yasin Twaibu (19) Dada wa Kazi Anayetuhumiwa Kutaka Kumuua Mtoto Wake Mchanga

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza, Machi 9, 2026, limemfikisha katika Mahakama ya Wilaya ya Ilemela, Faima Yasin Twaibu (19), mkazi wa Bulyehele, kwa tuhuma za kujaribu kumuua mtoto mchanga.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Christian Mwalimu, upande wa Jamhuri ukiongozwa na Wakili wa Serikali Evance Kaiza akisaidiana na Clara Muhando, ulidai kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Desemba 25, 2025 katika Mtaa wa Bulyehele, Wilaya ya Ilemela, baada ya kujifungua na kisha kumtupa mtoto juu ya paa la nyumba akidaiwa kuwa na lengo la kumuua.

Katika shauri namba 5112/2026, mshtakiwa anakabiliwa na shtaka moja la jaribio la kuua, kinyume na Kifungu cha 211(b) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16, kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2023. Akijibu swali la mahakama, mshtakiwa alidai alifanya hivyo kwa hofu mwajiri wake kugundua kuwa alikuwa mjamzito na amejifungua.

Mahakama ilisema kosa hilo lina dhamana, lakini mshtakiwa alishindwa kutimiza masharti ya kuwa na wadhamini wawili wenye vitambulisho vya Taifa na kusaini dhamana ya shilingi milioni tatu kila mmoja, hivyo kupelekwa rumande. Mtoto huyo, mwenye umri wa miezi miwili na wiki mbili, anaendelea kuwa salama chini ya uangalizi wa Maafisa Ustawi wa Jamii.

Shauri hilo limeahirishwa hadi Machi 23, 2026, litakapotajwa tena kwa ajili ya hatua za awali za usikilizwaji.

Leave a Comment