
Vanessa Trump, aliyewahi kuwa mke wa Donald Trump Jr, amethibitisha kupatikana na ugonjwa wa saratani ya matiti kupitia taarifa aliyochapisha kwenye mitandao ya kijamii.
Katika ujumbe wake wa Instagram, Vanessa alisema kuwa hakutarajia kupata taarifa hiyo, lakini kwa sasa anafanya kazi kwa karibu na madaktari wake kupanga mpango wa matibabu.
“Sikutarajia kupata habari kama hii, lakini ninafanya kazi na timu yangu ya kitabibu kupanga matibabu,” aliandika.
Vanessa Trump alieleza kuwa tayari amefanyiwa utaratibu wa kitabibu mapema wiki hii na kwa sasa anaendelea na hatua za awali za matibabu huku akiomba faragha kutoka kwa umma ili aweze kuzingatia afya yake na uponaji.

Aliongeza kuwa anapata nguvu kupitia msaada wa familia yake, watoto wake, pamoja na watu wa karibu.
Taarifa yake imepokea ujumbe mwingi wa pole na maombi ya uponaji, ikiwemo kutoka kwa Ivanka Trump, ambaye alimwombea afya njema na nguvu katika kipindi hiki kigumu.
Vanessa na Donald Trump Jr. walifunga ndoa mwaka 2005 katika jumba la Mar-a-Lago na baadaye kutengana mwaka 2018. Wana watoto watano pamoja.
Vanessa, ambaye awali alikuwa mwanamitindo, alikutana na Trump Jr. kupitia baba yake, Donald Trump, mwanzoni mwa miaka ya 2000.
Kwa mujibu wa takwimu za afya, saratani ya matiti ni miongoni mwa magonjwa yanayowapata wanawake wengi duniani, lakini matibabu ya mapema yanaweza kusaidia kuongeza nafasi ya kupona.
Kwa sasa, Vanessa ameomba muda na faragha wakati akiendelea na matibabu yake.