×

Rais Samia Asema Wananchi Bado Hawana Imani Kubwa na Polisi (Picha +Video)

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema bado kuna kazi kubwa ya kufanyika ili wananchi waweze kuliamini zaidi Jeshi la Polisi na kuliona kama sehemu salama ya kupata msaada wanapokumbana na changamoto mbalimbali.

Rais Samia amesema hayo baada ya kutazama video mtandaoni iliyokuwa ikielezea kiwango cha kukubalika kwa majeshi ya polisi barani Afrika miongoni mwa wananchi wake.

Akizungumza kuhusu taarifa hiyo, Rais Samia amesema nchi iliyoonekana kuongoza katika viwango vya kuaminiwa ilikuwa na asilimia 25 huku Tanzania ikitajwa kuwa na asilimia 12 pekee, hali ambayo imeonyesha umuhimu wa kuendelea kuboresha mahusiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

Amesisitiza kuwa ni muhimu kwa vyombo vya usalama kuhakikisha wananchi wanajenga imani navyo na kuviona kama sehemu ya msaada na ulinzi wakati wote wanapopata matatizo au wanapohitaji huduma za kiusalama.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama wakati wimbo wa Taifa ukiimbwa kwenye uwanja wa Chuo cha Taaluma ya Polisi, Kurasini Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Mei, 2026.
Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan akikagua Gwaride lililoandaliwa na Jeshi la Polisi kabla ya kuhitimisha Mafunzo ya Maafisa na Wakaguzi Wasaidizi wa Jeshi hilo, Kurasini Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Mei, 2026.
Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia akitoa vyeti kwa Wahitimu waliofanya vizuri kwenye Mafunzo ya Maafisa na Wakaguzi Wasaidizi wa Polisi, kozi namba 1 ya mwaka 2025/2026 katika Chuo cha Taaluma ya Polisi, Kurasini Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Mei, 2026.

 

Leave a Comment