
Iran imetangaza rasmi ratiba ya mazishi ya Kiongozi Mkuu wa zamani wa nchi hiyo, Ayatollah Ali Khamenei, ambaye alifariki dunia baada ya kuuawa katika mashambulizi ya anga yaliyofanywa na Marekani na Israel mwishoni mwa Februari mwaka huu.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali ya Iran, shughuli za mazishi zitaanza jijini Tehran Julai 4 kabla ya kuendelea katika mji mtakatifu wa Qom Julai 7 na kuhitimishwa kwa mazishi rasmi Julai 9 katika mji wa Mashhad, alikozaliwa Khamenei.
Khamenei, aliyekuwa na umri wa miaka 86, aliiongoza Iran kwa zaidi ya miaka 36 na alikuwa mmoja wa viongozi wenye ushawishi mkubwa katika siasa za Mashariki ya Kati. Wakati wa uongozi wake, Iran iliimarisha ushawishi wake wa kijeshi na kisiasa kupitia makundi washirika katika eneo hilo huku ikiendelea kuwa mpinzani mkubwa wa sera za Marekani.
Mashambulizi yaliyomuua yaliharibu makazi yake makuu mjini Tehran. Baada ya kifo chake, mwanawe mwenye umri wa miaka 56, Mojtaba Khamenei, alitangazwa kuwa mrithi wa nafasi ya Kiongozi Mkuu wa Iran.
Wakati huo huo, juhudi za kidiplomasia kati ya Iran na Marekani zinaendelea, huku Waziri Mkuu wa Pakistan, Shehbaz Sharif, akisema kuwa pande hizo mbili zimefikia makubaliano ya awali ya amani baada ya zaidi ya miezi mitatu ya vita na zinatarajiwa kusaini mkataba wa awali katika muda mfupi ujao.