×

Trump Amlinda Infantino, Asema Kumuondoa FIFA Ni “Kosa Kubwa”

WASHINGTON, Agosti 11, 2026 — Rais wa Marekani, Donald Trump, ametoa uungwaji mkono kwa Rais wa Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA), Gianni Infantino, ambaye anakabiliwa na presha kubwa kutoka ndani ya uongozi wa soka duniani.

Trump amesema itakuwa “kosa kubwa” kwa FIFA hata kufikiria kumuondoa Infantino katika nafasi hiyo, akimtaja kuwa kiongozi aliyefanya vizuri katika kuendesha shughuli za soka duniani.

Kupitia ujumbe wake kwenye mitandao ya kijamii, Trump amesema Infantino ni kiongozi “mzuri sana” na kwamba ameongoza Kombe la Dunia la 2026 ambalo, kwa mujibu wake, limekuwa na mafanikio makubwa zaidi kuwahi kutokea.

Trump amesema iwapo Infantino ataondoka, Kombe la Dunia na shughuli za FIFA huenda zisifikie kiwango kilekile cha mafanikio na faida.

Kauli hiyo imekuja wakati Infantino akikabiliwa na upinzani kutoka kwa baadhi ya mashirikisho makubwa ya soka duniani kufuatia mpango wa Fifa Forward Enterprise (FFE) uliositishwa.

Mpango huo ulipendekeza kuanzishwa kwa kampuni mpya ambayo ingesimamia haki za kibiashara na tiketi za mashindano ya FIFA, yakiwemo Kombe la Dunia, huku asilimia 21 ya kampuni hiyo ikitarajiwa kuuzwa kwa kampuni binafsi ya uwekezaji.

UEFA, Concacaf na Shirikisho la Soka la Asia (AFC) zimekosoa vikali mpango huo, zikimtuhumu Infantino kwa kuvunja imani kupitia kile walichokiita udanganyifu.

Katika barua ya pamoja, mashirikisho hayo yalisema uaminifu unapovunjwa na mtu kuweka maslahi yake binafsi juu ya taasisi iliyompa mamlaka, basi wajibu wake kwa taasisi hiyo huwa umeachwa.

UEFA pia imetishia kususia mashindano yote yanayoandaliwa na FIFA pamoja na kuchukua hatua za kisheria kuhusu mpango huo ulioshindikana.

Taarifa zinaeleza kuwa kumekuwa na mazungumzo ya awali kati ya UEFA, Concacaf na AFC kuhusu uwezekano wa kuanzisha mashindano mbadala iwapo Infantino ataendelea kubaki madarakani, ingawa hakuna mazungumzo rasmi yenye kina ambayo yameanza.

Uhusiano kati ya Trump na Infantino umekuwa wa karibu. Infantino alimtunuku Trump FIFA Peace Prize ya kwanza mnamo Desemba 2025.

Trump pia aliwahi kusema mwishoni mwa Julai kwamba hakuwa amezungumza na Infantino kuhusu mpango wa FFE wakati suala hilo lilipoibuka.

Kwa sasa, kauli ya Trump imeongeza uzito wa kisiasa kwenye mgogoro unaoendelea ndani ya soka la dunia, huku shinikizo kwa Infantino likiendelea kutoka kwa baadhi ya viongozi wa mashirikisho ya soka.

Leave a Comment