
Tottenham Hotspur imekamilisha usajili wa winga wa Brazil, Savinho, kutoka Manchester City kwa ada ya awali ya takribani TSh bilioni 262.5, sawa na pauni milioni 75, huku thamani ya usajili huo ikitarajiwa kufikia karibu TSh bilioni 297.5 iwapo vigezo vya nyongeza vitatimia.
Savinho, mwenye umri wa miaka 22, ambaye sasa ameamua kutumia jina Sávio, amesaini mkataba wa muda mrefu na Tottenham katika hatua inayolenga kuimarisha kikosi cha Spurs.
Kocha wa Tottenham, Roberto De Zerbi, amesema ujio wa Sávio utaongeza nguvu, ubunifu na uwezo wa kuwachanganya mabeki wapinzani katika maeneo ya pembeni.
Msimu uliopita akiwa Manchester City, Sávio alicheza mechi 24 za Premier League, akianza michezo saba. Kwa ujumla, alicheza mechi 84 akiwa na City na kufunga mabao saba.
Usajili huo unaifanya Tottenham kutumia zaidi ya TSh trilioni 1.05 katika dirisha hili la usajili, ikiwa ni sehemu ya mpango wa De Zerbi wa kujenga upya kikosi.
Spurs pia wamehusishwa na mshambuliaji mwingine wa Manchester City, Omar Marmoush, huku klabu hiyo ikiendelea kutafuta nyongeza zaidi katika kikosi chake.
Kwa upande wa Manchester City, mauzo ya Sávio yanaweza kuwa rekodi ya mauzo ya klabu hiyo iwapo thamani ya uhamisho itafikia £85 milioni, sawa na takribani TSh bilioni 297.5.
Rekodi ya awali ya mauzo ya City inatajwa kuwa ya mshambuliaji Julian Alvarez, aliyehamia Atlético Madrid mwaka 2024 kwa ada ya £82 milioni, sawa na takribani TSh bilioni 287.
Usajili wa Sávio ni sehemu ya mpango wa Tottenham wa kujenga kikosi chenye ushindani zaidi baada ya kumaliza msimu uliopita katika nafasi ya 17, huku De Zerbi akilenga kuirejesha Spurs katika ushindani wa nafasi za juu.
Stori na Erick Elibariki | GPL -TUDACO