The House of Favourite Newspapers

Buriani Makongoro Oging’

0

makongoroMwandishi Makongoro Oging’ enzi za uhai wake.

“Makongoro Oging’ amefariki dunia,” yalikuwa ni maneno yaliyopenya masikioni mwangu kutoka kwa Oscar Ndauka, Mhariri Kiongozi wa Global Puplishers alipofika nyumbani kwangu Jumamosi usiku wa Mei 21, mwaka huu akiwa na Sifael Paul, Mhariri wa Gazeti la Ijumaa Wikienda.

Nilipigwa na butwaa kusikia habari hiyo ambayo kama ningekuwa na matatizo ya kiafya ningeweza kupata presha, huku mke wangu akishikwa na mshangao na akihoji kama vile hakusikia: “Makongoro kafariki duni?”

tar 14.8.2015 Makongoro akimuhoji mke wa aliyekuwa askari wa gereza la Dondwe Pwani ambaye aliuawa katika uvamizi wa kituo cha Stakishari, Picha na Richard Bukos (1)Tar 14.8.2015 Makongoro akimuhoji mke wa aliyekuwa askari wa gereza la Dondwe Pwani ambaye aliuawa katika uvamizi wa kituo cha Stakishari, Picha na Richard Bukos.

Nilimuona akifuta machozi kwa khanga, kisha nami nikachukua kitambaa na kufuta machozi. Tulizungumza mengi hadi saa nane usiku kupanga tufanyeje kesho kukicha baada ya kuzungumza na mke wa Makongoro usiku huo huo na kututhibitishia habari hiyo.

Jina la Makongoro Oging’ siyo geni kwa watu wanaofuatilia habari hasa wasomaji wa magazeti ya Global Publishers hususan Gazeti la Uwazi.

Ni juzi tu aliniletea fomu zake za kutaka press card na alipoijaza ikaonesha kuwa yumo ndani ya tasnia ya habari kwa miaka 21 sasa, hivyo kutosha kusema kwamba ni mkongwe katika fani hii.

Makongoro alikuwa mahiri wa kuandika habari za uchunguzi kwani  mwaka 2004 alipewa tuzo ya mwandishi bora wa habari hizo, iliyotolewa na Chuo cha Uandishi wa Habari cha Royal Tanzania kilichopo Ubungo, Dar es Salaam.

Miongoni mwa watu waliotunukiwa tuzo siku hiyo ni Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Betty Mkwasa pamoja na waandishi wa habari wengine ambao majina yao siwezi kuyakumbukwa kwa sasa.

Alistahili kwa sababu Makongoro alipokuwa kazini hakuwa na mchezo. Alikuwa akifuatilia habari za uchunguzi kwa kina. Nakumbuka siku moja aliandika habari moja ya udhalilishaji uliofanywa na vijana fulani baada ya kumteka msichana mmoja na kumpiga sana kisha kumvua nguo.

Sakata hilo lilifika jeshi la polisi wakati huo Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum, Kamishna Mstaafu Alfred Tibaigana akiwa madarakani alinipigia simu na kunitaka niende na Makongoro ofisini kwake ‘ sentro’.

Tulipofika tu akatuona tupo kwenye korido akasema kwa sauti, “Kamanda Zombe ( Abdallah), watu wa Uwazi wamefika, Makongoro uliyekuwa ukimtafuta huyu hapa, kaja na bosi wake.”

Zombe aliyekuwa mkuu wa upelelezi wa polisi wa kanda maalum ya Dar es Salaam wakati ule, alikuwa kwenye chumba kimoja na aliposikia sauti ya bosi wake alitoka na kutulaki huku akitukaribisha.

“Karibuni sana.”

“Ahsante.”

“Tumekuwa tukifuatilia gazeti lenu la Uwazi na habari ya wiki hii ipo mezani kwangu naomba mtusaidie mawili matatu,” alisema Zombe.

Baadaye alitukabidhi kwa askari mmoja wa upelelezi ambaye namkumbuka kwa jina moja tu la Judi ili tufanye naye mahojiano.

Judi alituchukua hadi ofisini kwake na kuanza kunihoji mimi kwa dakika chache kama mhariri wa habari ile na baadaye akaanza kumhoji Makongoro ambaye alichukua muda mrefu kutokana na mambo mengi ambayo alikuwa anayajua kuhusiana na habari ile.

Baada ya mahojiano yale Kamanda Tibaigana alituita ofisini kwake na kusifia umahiri wa Makongoro katika kuandika habari za uchunguzi na akasema huwa zinamsaidia sana katika uchunguzi wa tuhuma mbalimbali ambazo zinawafikia.

Tangu siku hiyo Makongoro Oging akawa rafiki wa Tibaigana na Zombe pamoja na askari wengine wengi pamoja na mawakili akiwemo Mabere Marando hali iliyofanya awe mahiri wa kuandika habari zinazohusu watuhumiwa mbalimbali.

Ilikuwa siyo rahisi kwa Makongoro kwenda kwenye kituo fulani cha polisi na kukosa ushirikiano anapofuatilia jambo kutokana na uhusiano mzuri alioujenga na askari hao hata wale wa Magereza na Kikosi cha Zima Moto.

Kwa upande wa wagonjwa katika hospitali mbalimbali, Makongoro alikuwa akiwaandika sana na kuwaombea misaada kwa wasomaji wa Gazeti la Uwazi na alifanikiwa kuwawezesha baadhi yao kupelekwa nje ya nchi kutibiwa kwa kuchangiwa na wasomaji.

Wengine walipelekwa India, wengine hospitali za humu ndani na kubadili maisha yao baada ya kutibiwa na kupona kutokana na kalamu yake aliyoitumia kwa manufaa ya jamii.

Wapo watu ambao walikuwa na maisha duni lakini Makongoro kwa kutumia kalamu yake aliandika habari zao na baadhi yao kufanikiwa kujengewa nyumba za kisasa.

Kwa upande wa wanafunzi, Makongoro hakuwaacha nyuma, nao alikuwa akiwafuata na kuandika matatizo yao. Wapo waliokuwa wakikwama kimasomo kutokana na wazazi wao au walezi wao kushindwa kuwalipia ada, mwandishi huyu aliandika habari zao na baadhi yao wakafadhiliwa na kusoma hadi chuo kikuu.

Makongoro hakuwa mchoyo wa fani yake, nimemshuhudia zaidi ya miaka 15 akiwafundisha waandishi chipukizi habari za uchunguzi na kuwa wa kutumainiwa katika chumba cha habari.

Alikuwa akipenda kuwafundisha uandishi wa uchunguzi waandishi chipukizi kivitendo kwani baadhi yao alikuwa akiongozana nao kwenye matukio na kuwafundisha kivitendo jinsi ya kufuatilia habari za uchunguzi alizokuwa akiziandika enzi za uhai wake.

Kazi yake ilimfanya ajulikane sehemu nyingi, kama vile ndani ya majeshi yetu yote, katika hospitali kubwa, mitaani na hata kwenye mashirika na taasisi za umma na zile binafsi.

Alikuwa jasiri kwa kufuatilia jambo bila woga na ndiyo maana mpaka anaaga dunia Jumamosi saa moja jioni hatukuwahi kuwa na kesi kwenye gazeti iliyosababishwa naye.

Makongoro ameacha mjane na watoto watatu. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina.

KUNUNUA NA KUSOMA MAGAZETI YA GLOBAL PUBLISHERS ONLINE, INGIA HAPA==>VODACOM M-PAPER APP

*********

JIUNGE NA SOCIAL MEDIA ZETU

KWA HABARI ZA KITAIFA, KIMATAIFA, MASTAA NA MIKASA YA KUSISIMUA

INSTAGRAM: @Globalpublishers

ERIC SHIGONGO INSTAGRAM: @ericshigongo

TWITTER: @GlobalHabari

FACEBOOK: @GlobalPublishers

SUBSCRIBE YOU TUBE: Global TV Online

GLOBAL TV ONLINE: www.globaltvtz.com

HADITHI ZA KUSISIMUA NA MBINU ZA UJASIRIAMALI, ERIC SHIGONGO FACEBOOK PAGE:@shigongotz

Leave A Reply