×

Dude aufungukia mwezi mtukufu

dude1.jpgWIKI hii kwenye safu yetu ya maswali 10 tunaye msanii nguli wa filamu nchini Kulwa Kikumba almaarufu kama ‘Dude’ anayezungumza na Mwandishi Wetu Gabriel Ng’osha.         

Ijumaa: Nini unapenda kufanya ndani ya mwezi huu mtukufu?

Dude: Napenda sana kupumzika nyumbani hata kwa kazi zangu huwa nachukua likizo.

Ijumaa: Ni futari ipi ambayo unapenda kufuturu baada ya swaumu kali?

Dude: Ya muhogo au magimbi iliyoungwa na karanga, si unajua mimi Mnyamwezi, njugu, maharage, tambi ni mara moja moja.

Ijumaa: Nani anakuandalia futari wakati kiimani haupaswi kuwa karibu na mkeo kwa sababu hamjafunga ndoa?

Dude: Tuna mfanyakazi na watoto wangu ni wakubwa hivyo wananiandalia futari vizuri tu.

Ijumaa: Wakati huo mkeo anakuwa yuko wapi?

Dude: Anakuwa kazini kwake, tuna kiduka na saluni ila pia anakuwa amefunga.

Ijumaa: Nini cha kujifunza kwenye mwenzi huu wa Ramadhani?

Dude: Kila kitu kinatulia, hakuna ujinga unaofanyika, hata vibaka huwa wanatulia, natamani hali hii iwepo siku zote.

Ijumaa: Unafaidika nini kufunga?

Dude: Mwenyezi Mungu anasema unapofunga unapata afya njema ni mwezi wa kufanya toba na kujisahisha kwa yale yote uliyoyafanya mwaka mzima na pia unajipatia thawabu.

Ijumaa: Vipi kuhusu biashara ya filamu kwa muda huu?

Dude: Mara nyingi wasanii huwa tunaandaa filamu za mwezi mtukufu ila mwaka huu sikufanikiwa kuandaa filamu yangu kwa sababu nilikuwa na kazi nyingine.

Ijumaa: Nini ushauri wako kwa wasanii kuhusu kufunga?

Dude: Ni mwezi mmoja basi tuutumie msimu huu wa mfungo vizuri kutubu madhambi yetu, kwani Mungu katupa uhai wa kufanya kazi mwaka mzima.

Ijumaa: Unafanya nini kuwasaidia wahitaji kipindi hiki cha mfungo?

Dude: Ninapokuwa na nafasi najitoa kwa chochote na huwa sisubiri mpaka Ramadhani na ndiyo maana kipindi f’lani nilienda kwa walemavu wa ngozi na kwingineko.

Ijumaa: Wengi wanasema mwezi huu ni mgumu sana ni kweli?

Dude: Hauna ugumu wowote ni kama likizo anayoipata mfanyakazi wa kampuni au taasisi yoyote ile duniani.

Leave a Comment