WIKI hii tunaye msanii wa Muziki wa Kizazi Kipya, Dayna Nyange anayetamba na Wimbo wa Angejua. Yupo hapa kujibu maswali 10 aliyoulizwa na Mwandishi Wetu Gabriel Ng’osha. Fuatilia…
Ijumaa: Shabiki wako angependa kwanza kujua maisha yako ya kimapenzi yakoje?
Dayna: Mimi ni mama wa mtoto mmoja, bado sijaolewa.
Ijumaa: Hujaolewa ina maana una mchumba, mpenzi au upoupo tu?
Dayna: Ninaye mpenzi ambaye siku Mungu akipenda huenda tukawa mwili mmoja.
Ijumaa: Unamaanisha yule uliyezaa naye au mwingine?
Dayna: Niliyezaa naye niliachana naye kitambo, ninaye mwingine ambaye tunapendana kwa dhati.
Ijumaa: Kuna tetesi kuwa anayekuweka mjini ni kigogo mmoja wa serikalini, hilo likoje?
Dayna: Kama nilivyosema, nina mpenzi wangu, hivi ni kigogo gani wa kuniweka mjini jamani?
Ijumaa: Kwa hiyo unataka kusema anayekupa jeuri ya kula, kuvaa, kumsomesha mwanao ni huyo mpenzi wako au unamaanisha muziki unakulipa sana?
Dayna: Si haba nashukuru Mungu kwani kupitia muziki naweza kumsomesha mwanangu na kufanya mambo mengine ya kimaendeleo.
Ijumaa: Mbona inaonekana kama vile nyota yako haing’ari kihivyo kwenye gemu?
Dayna: Ni mtazamo wa watu kwani binafsi ni msanii wa kitambo sana wa kike, nimedumu na ninaona muziki wangu unapiga hatua.
Ijumaa: Wimbo wako wa Nivute Kwako ulifanya vizuri sana, unadhani unaweza kutoa wimbo mkali kama huo tena?
Dayna: Ni kweli Nivute Kwako ilifanya poa ila haikunipa mafanikio kivile lakini Angejua imefanya vyema zaidi. Wanaofuatilia muziki wa Bongo wanajua hilo.
Ijumaa: Changamoto gani unakumbana nazo kwenye gemu?
Dayna: Ni nyingi sana ila kikubwa ni kukomaa, wapo wanaojaribu kubana lakini si unajua Mungu akikupangia hakuna wa kuzuia, unapasua tu!
Ijumaa: Kwa jinsi unavyoona muziki wa Bongo ulivyo, unadhani unaweza kumruhusu mwanao akikua awe msanii?
Dayna: Hiyo ni mipango ya Mungu, kikubwa asome kwanza kisha kipi atafanya akili yake itamtuma.
Ijumaa: Umesema una mpenzi, hivi siku moja ukimfumania utachukua uamuzi gani?
Dayna: Namuamini sana, sidhani kama hilo linaweza kutokea. Ila kwa sababu siwezi kuusemea moyo wake, siku ikitokea nitajua uamuzi wa kuchukua kwa wakati huo.