Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema, akikabidhi ripoti ya uongozi wa soko kwa mwenyekiti mpya wa bodi ya soko hilo, Henry Massaba.
…Akiangalia baadhi ya samaki waliokuwa wakiuzwa na wafanyabiashara wa samaki wa soko hilo.
…Akizungumza jambo katika hafla hiyo.
Mmoja wa wafanyabiashara wa samaki akimwelezea changamoto mbalimbali zinazowakabili.
MKUU wa Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam, Sophia Mjema, ameitaka bodi mpya ya soko la samaki (Feri) jijini Dar es Salaam kuhakikisha linageuza sura ya sasa ya soko hilo na kuwa soko la kimataifa kwa kutengenezewa miundombinu na mazingira mazuri ili kuwavutia watu wanaoingia eneo hilo.
Hayo ameyasema leo sokoni hapo alipokuwa mgeni rasmi kukabidhi ripoti ya uongozi wa soko hilo kwa bodi hiyo mpya.
Amesema ili soko hilo liweze kuwa la kimataifa viongozi wa soko hilo wanatakiwa kuhakikisha hakuna vibaka wanaoshinda ndani ya soko hilo na kuwataka viongozi na uongozi wa bodi kulizungushia uzio kwa nyuma ili kuondokana na makundi maovu yanayoshinda yamekaa maeneo hayo pasipokuwa na kazi maalum.
Alieleza kuwa haamini kwamba soko hilo haliwezi kuondokana na harufu mbaya inayosikika eneo la Feri mtu anapokaribia eneo hilo kwani harufu hiyo inatokana na mazingira ya uchafu na kuwataka viongozi hao kuhakikisha wanaiondoa harufu hata kwa kuweka dawa katika mazingira yanayostahili.
Aidha alifafanua kuwa si tu kwamba soko hilo linatembelewa na wakazi wa Dar es Salaam tu bali na watu kutoka mikoa mingine na mataifa ya nje kufanya utalii wao, hivyo linapaswa kuwa kivutio.
Vilevile ameitaka bodi kuhakikisha wanaongeza mapato yanayokusanywa ya kodi tofauti na ilivyo hivi sasa ambapo alisema kuna wafanyabiashara takribani elfu nne hivyo mapato yanayopatikana hayaendeni na idadi kamili.
Na Denis Mtima/GPL
Comments are closed.