Baba mzazi wa marehemu Thomas Mashali, Malifedha Mashali akitoa ufafanuzi juu ya msiba huo.
BABA mzazi wa aliyekuwa bondia wa ngumi za kulipwa, Thomas Mashali ‘Simba asiyefugika’, Malifedha Christopher Mashali amesimulia namna alivyoguswa na kifo cha mwanaye huyo kilichotokea usiku wa kuamkia leo Kimara jijini Dar.
Mmoja wa majirani wa marehemu Mashali akimzungumzia jinsi alivyomfahamu bondia huyo.
Akizungumza na mtandao huu, nyumbani kwake Tandale kwa Mtogole jijini Dar, mzee Mashali alisema taarifa za kifo cha mwanaye alizipata leo alfajiri kupitia kwa vijana watatu ambao walifika nyumbani hapo pasipo kujitambulisha majina yao na kumfikishia taarifa kuwa Mashali kafikikishwa katika Hospitali ya Sinza (Palestina) akiwa hajitambui kutokana na kipigo alichopigwa na watu wasiojulikana.
Watoto wa Marehemu Mashali wakiwa katika huzuni kwenye picha ya pamoja na shangazi yao aitwaye Josephine Mashali (wa kwanza kushoto) nyumbani kwao Tandale jijini Dar.
“Nilishtuka sana baada ya kuletewa taarifa kwamba Mashali kapigwa na watu wasiofahamika huko Kimara- Bonyokwa, taarifa waliniletea vijana watatu ambao hawakujitambulisha wala kukubali kuelezea kwa kirefu zaidi ya kusema kuwa mwanangu yupo Hospitali ya Palestina akiwa hajitambui kufuatiwa kupigwa na watu ambao hawajulikani.
Ndugu, jamaa na marafiki wakiwa msibani kwa baba mzazi wa marehemu Mashali.
“Baada ya taarifa hizo niliwasiliana na ndugu zake wengine akiwemo dada yake ambao walikwenda Palestina kufuatilia lakini walimkuta ameshapewa rufaa ya kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili ingawa tayari pale walishaelezwa alikuwa ameshafariki dunia kutokana na kupigwa sana kichwani.
Waandishi wa habari za michezo wa Gazeti la Championi, Wilbert Molandi (kushoto) na Sweetbert Lukonge (katikati) wakifanya mahojiano na dada wa marehemu Mashali aitwaye Josephine.
“Kuhusu suala la mazishi bado hatujajua lini tutazika kwa sababu maiti imehifadhiwa Muhimbili, halafu kuna mambo ya uchunguzi wa kipolisi yanatakiwa yafanyike na baadaye ndiyo tutajua lini tutazika. Nimeumizwa na kifo chake kwa sababu mara ya mwisho niliongea naye jana katika simu,” alisema baba Mashali.
Taswira ya nyumbani kwa baba mzazi wa marehemu Thomas Mashali, Tandale kwa Mtogole jijini Dar.
Naye dada wa marehemu, Josephine Mashali alisema amepokea taarifa za kifo cha kaka yake kwa masikitiko makubwa na anamuomba Mungu ampumzishe kwa amani katika nyumba yake ya milele.Baba mzazi wa marehemu Thomas Mashali, Malifedha Mashali akizungumza na Global TV Online kuhusiana na msiba huo akiwa nyumbani kwake Tandale.
Marehemu Mashali ameacha jumla ya watoto watano wote wakiwa ni wa kike.
Bondia Thomas Mashali enzi za uhai wake.
Na Denis Mtima/Gpl