
RAIS mstaafu wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete, amempongeza aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, kwa kazi nzuri aliyoifanya ndani ya chama wakati wa uongozi wake huku akimtakia kila la kheri katika maisha yake baada ya kustaafu wadhifa wake huo.
Kikwete amempongeza pia Dkt. Bashiru Kakurwa kwa kuteuliwa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) kuwa Katibu Mkuu wa chama hicho kuchukua nafasi ya Kinana.
Aidha, amempongeza Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli kwa kukiendesha vyema chama hicho huku akiwataka wanachama wake waendeleze umoja wao.
Kupitia akaunti yake ya Twitter, Kikwete ameandika;
“Kwa heri Kinana. Hongera kwa kazi nzuri. Daima tutakukumbuka. Hongera Bashiru. Nakutakia kila la heri. Hongera @ccm_tanzania , hongera Mwenyekiti @MagufuliJP Umoja ni Ushindi, Kidumu Chama Cha Mapinduzi !”

Mnamo Mei 28, 2018, Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, iliridhia maombi ya Kinana kustaafu nafasi yake hiyo ya Ukatibu Mkuu wa Chama ambapo chama hicho kilimteua Dkt. Bashiru Ali Kakurwa kuchukua nafasi hiyo.


Comments are closed.