The House of Favourite Newspapers

Baada ya Mapito Mazito,Hawa nitarejea amtamani Diamond

ANAITWA Hawa Mayoka lakini wengi wanapenda kumuita Hawa Nitarejea. Mwanadada huyu amepitia wakati mgumu baada ya kuugua lakini Mungu akamsimamisha tena.

Ukibahatika kuzungumza naye lazima atakuambia anamshukuru sana Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ ambaye mbali na kwamba waliwahi kufanya kazi pamoja lakini ndiye aliyefanikisha matibabu yake na leo hii yuko poa kabisa.

Msanii huyu aliyeonesha uwezo wa kuimba kwenye nyimbo zake za hivi karibuni za Mawazo na Kucheka amefanya mahojiano na safu hii na kusema:

“Sasa nina maisha mapya, namshukuru sana Diamond kwa kunishika mkono. Siwazi suala la ndoa kwa sasa, nayaangalia maisha yangu. Hapa nilipo natamani kupata menejimenti ya kusimamia kazi zangu ili niweze kufikia ndoto zangu,” anaeleza Hawa huku akionekana ni mwenye nguvu na ari mpya.

Ili kujua mengi kuhusu msanii huyu ambaye wengi walikuwa wamemkatia tamaa, fuatilia hapa chini…

Showbiz: Hali yako kwa sasa ikoje tangu urudi kutoka India?

Hawa: Kwa kweli namshukuru sana Mungu, nipo sawa kabisa kwa sababu sasa hivi nakula na kulala vizuri bila shida yoyote.

Showbiz: Vipi kuhusu hali ya mama yako, maana kipindi unaumwa alichanganyikiwa sana.

Hawa: Hali ya mama yangu kwa sasa ni nzuri, huwezi amini siku hizi ana furaha mno kwa sababu ananiona binti yake niko vizuri.

Showbiz: Tuzungumzie wimbo wa Mawazo, hivi ile aidia ilikujakujaje?

Hawa: Unajua kipindi nipo Soba naumwa, kuna siku nililala nikaota nimepona, sasa nilivyoamka ghafla nikapata aidia ya huo wimbo wa Mawazo, kwa hiyo nikamuomba ruhusa Pili Massana (Msimamizi wa kituo cha matibabu kwa waathirika wa dawa za kulevya) akaniruhusu kwenda studio kurekodi. Kwa hiyo huo wimbo niliuimba tangu kipindi kile bado nina tumbo kubwa linanisumbua na nimeutoa kipindi hiki kama shukurani kwa Watanzania.

Showbiz: Ndio tuseme umeshaingia rasmi kwenye gemu au ulikuwa unabipu tu?

Hawa: Sijabipu ila nimeingia rasmi kwa sababu hapa nilipo tayari nina nyimbo saba bado sijazirekodi.

Showbiz: Nani anakusimamia kwa sasa kwenye muziki wako?

Hawa: Najisimamia mwenyewe, bado sijapata menejimenti na sijapata kwa

sababu wengi wao hawaniamini kama naweza kufanya kazi vizuri.

Showbiz: Nini unakifanya ili uaminike kwamba unaweza kufanya kazi freshi kabisa?

Hawa: Kikubwa naomba mameneja waniamini, uwezo wa kuimba ninao, wakinipa nafasi wataona ambavyo

 

 

sitawaangusha.

Showbiz: Tangu umetoa huo wimbo wako umewahi kuitwa kwenye shoo yoyote?

Hawa: Hapana, sijawahi kuitwa kwenye shoo yoyote japo natamani sana nipate nafasi ili nikaonyeshe uwezo wangu.

Showbiz: Ulijisikiaje baada ya kupanda jukwaani na kupafomu pamoja na Diamond?

Hawa: Nilijisikia vizuri sana sijui hata nisemeje, maana alinisapoti na kunipokea vizuri, alinionyesha heshima ya hali ya juu, naomba Mungu ampe maisha marefu, hakika ni mtu poa sana.

Showbiz: Unatamani siku moja ufanye naye tena kolabo?

Hawa: Hakika miongoni mwa wasanii wa kiume Bongo, namtamani sana Diamond. Ipo siku nitamshirikisha hili, najua hawezi kukataa kwa sababu najua hata mashabiki zetu wanatamani tena kuona kaz

yangu na yeye.

Showbiz: Kuna kipindi tetesi zilivuma kuwa una mpango wa kujiunga na Lebo ya WCB lakini mpaka sasa tunaona kimya, mpango wenu uliishia wapi?

Hawa: Sijawahi kuongea na WCB kuhusu kujiunga nao na wala wao hawajawahi kuniambia mimi, hayo maneno nadhani watu walijitungia, japo siku wakinihitaji kwenye lebo yao nitakubali.

Showbiz: Maisha yako ya kimapenzi kwa sasa yakoje? Una mtu?

Hawa: Sina mtu kwa sasa.

Showbiz: Wewe ni msichana mrembo, iweje ukose mtu wa kuinjoi naye?

Hawa: Wanaume wanaonipenda ni wengi tu lakini mimi mapenzi kwao sina kwa sababu nilishawahi kuumizwa sana, wengi wao ni waongo, hawana mapenzi ya dhati ndio maana nimeona bora nikae singo kuliko kuumia kila siku.

Showbiz: Vipi kama atatokea mwanaume mwenye nia nzuri ya kukuoa?

Hawa: Sidhani kama nitakuja kumuamini mwanaume yeyote yule, kwa sababu alishawahi kuja kijana mmoja mpaka nyumbani kwetu, akajitambulisha na kunitolea mahari, nikabadili mpaka dini kuwa Mkristo kwa sababu yake, lakini alikuja kuniacha vibaya, ndio maana mpaka leo hii siamini wanaume kabisa.

Showbiz: Jambo gani ambalo unalijutia sana kwenye maisha yako na hutamani lije kujirudia tena?

Hawa: Siijui kesho yangu ikoje, naishi kwa imani na kila ninachopitia au nilichowahi kukipitia kwenye maisha yangu naona ni funzo, naamini Mungu alinipitisha ili baadaye nije kuwa bora na mfano wa kuigwa kwenye jamii.

Showbiz: Unawaambia nini mashabiki zako?

Hawa: Nawapenda sana na naomba waendelee kunisapoti kwenye kazi zangu. Nimejipanga vizuri hivyo wategemee vitu vipya na safari hii nitawafanyia saprai

Comments are closed.