Hazard aweka rekodi Real
EDEN Hazard ameweka rekodi ya kuwa mchezaji ghali zaidi kuwahi kusajiliwa na Real Madrid baada ya kusaini kujiunga na timu hiyo juzi. Real Madrid ilitoa taarifa rasmi juzi ikieleza kuwa wamemalizana na Hazard na kuwa atajiunga na timu hiyo msimu ujao.
Klabu hiyo imemchukua winga huyo wa Chelsea kwa ada iliyogharimu kiasi cha pauni milioni 150 (Sh. bilioni 437),ambayo inamfanya kuwa mchezaji wa bei mbaya zaidi kuwahi kusajiliwa na timu hiyo.
Hazard, ambaye pia ameahidiwa mshahara wa pauni 400,000 (Sh. bilioni 1.6) kwa wiki, sasa ada yake imefanya ampiku Gareth Bale kama mchezaji ghali katika kikosi cha Real Madrid. Bale ndio alikuwa staa wa bei mbaya zaidi katika kikosi cha Real Madrid, ambapo alinunuliwa kwa kitita cha pauni milioni 88.8 (Sh. bilioni 258) kutoka Tottenham mwaka 2013.
Straika wa zamani wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo ndio alikuwa anashika nafasi ya pili baada ya uhamisho wake kugharimu pauni milioni 80 (Sh. bilioni 233) alipochukuliwa kutoka Manchester United mwaka 2009.
Kocha wa sasa wa Real Madrid, Zinedine Zidane ndio anakamata nafasi ya tatu kama staa ghali wa klabu hiyo kutokana na kununuliwa kwa ada ya pauni milioni 68.3 (sh. bilioni 177) kutoka Juventus mwaka 2001. Hazard amesaini mkataba wa kuchezea Real Madrid kwa miaka mitano na anatazamiwa kutambulishwa rasmi Alhamisi ijayo.
r
Comments are closed.