Kocha Amtaja Mrithi wa Mikoba ya Mkude Simba
KIWANGO bora kilichoonyeshwa na Said Ndemla kwa siku za hivi karibuni ndani ya Simba, kimemfungua mdomo kocha mkuu wa timu hiyo, Sven Vandenbroeck na kusema eneo la kiungo mkabaji limepata mchezaji mbadala kuelekea kwenye mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya FC Platinum.
Sven alisema kwenye michezo miwili kuanzia ule wa Azam Sports Federation Cup dhidi ya Majimaji wakishinda mabao 5-0, kisha na ule wa ligi kuu dhidi ya Ihefu wakishinda 4-0, Ndemla alifanya kazi kubwa ya kuimarisha safu ya ulinzi na ushambuliaji, hivyo anaamini kuwa mchezaji huyo atakuwa msaada kwenye kiungo cha ukabaji pindi watakapowavaa Platinum kwa kuwa amekuwa akifanya kazi yake vema bila kufanya makosa ya mara kwa mara.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Sven alisema Ndemla amekuwa na kiwango bora kwa siku za hivi karibuni, kwani amekuwa akitimiza majukumu yake kwa asilimia kubwa hasa kwenye eneo la kukaba na kushambulia kiasi ambacho kinampa wakati mzuri wa kuamua ni namna gani mchezaji huyo acheze kulingana na mahitaji yake kwenye mchezo husika.“
Ndemla amekuwa imara sana, anatimiza majukumu yake vema, tulimpa majukumu ya kukaba alifanya vizuri. Hiyo inanipa wakati mzuri sana wa kuandaa timu kuelekea kwenye mchezo wa marudiano, kwa kuwa eneo la kiungo mkabaji yupo mtu anayefanya kazi nzuri pia,” alisema Sven.
Stori: Issa Liponda,Dar es Salaam