The House of Favourite Newspapers

Kwa Chama Hili, Mtaikoma Yanga!

YANGA imepania acheni utani jamani, hii ni kutokana na usajili wanaoendelea kuufanya na tayari wamekamilisha saini za wachezaji tisa kati ya hao sita kutoka nje ya nchi na wawili wazawa.

 

Timu hiyo imemalizana na mastaa tisa ambao tayari wamesaini mikataba ya miaka miwili kila mmoja na kati ya hao yupo kipa wa Bandari, Farouk Shikalo, Erick Rutanga (Rayon Sports, Rwanda). Wengine ni Lamine Moro (Buildcon, Zambia), Issa Bigirimana ‘Walcot’ (APR, Rwanda), Maybin Kalengo (Zesco, Zambia), Abdul Aziz Makame (Mafunzo FC, Zanzibar), Ally Mtoni Sonso (Lipuli FC, Iringa).

 

Kwa usajili huo walioufanya Yanga umetokana na ripoti ya Kocha Mkuu wa timu hiyo Mfaransa, Mwinyi Zahera aliyoitoa kwa uongozi ili kuhakikisha anakisuka kikosi imara kitakachoipa mataji kwenye msimu ujao. Ushindani mkubwa wa namba unatarajiwa kuwepo kwelikweli msimu ujao kati ya hao nyota wapya waliosajiliwa na waliokuwepo katika timu hiyo iliyopanga kurejea anga za kimataifa.

Kwa kuanzia safu ya ulinzi, golini kipa namba moja anatarajiwa kuwa Shikalo ambaye yeye tofauti na uwezo wake mkubwa aliokuwa nao mkataba umeainisha kwamba lazima aanze kama hatakuwa majeruhi.

 

Beki wa kulia anatarajiwa kuwa, Paul Godfrey ‘Boxer’ aliyepandishwa kwenye huu uliopita na kuonyesha kiwango kikubwa ambaye ana uwezo mkubwa wa kulinda goli lake, kuanzisha mashambulizi ndani ya wakati mmoja ni kipenzi cha Zahera.

Beki wa kushoto ni Erick Rutanga anayeichezea Rayon Sports, yeye ni beki mbishi hana tofauti na Boxer lakini yeye ni mzuri zaidi kwa kupiga krosi na mabeki wa kati ni Lamine Moro ambaye yeye ana umbile kubwa na uwezo wa kupiga vichwa, pia ni mtemi ngumi mkononi hana tofauti na Kelvin Yondani atakayecheza naye pamoja namba 4 na 5.

 

Kiungo mkatabaji yaani pale namba sita atasimama Makame. Huyu ameletwa kwa ajili ya kumpunguzia kazi ya kukaba Feisal Salum ‘Fei Toto’ na Papy Tshishimbi ambao msimu huu uliomalizika walikuwa wakitumia muda mwingi katika kukaba kuliko kuchezea mpira, hivyo ujio wake kutaimarisha kikosi hicho na kuwa tishio.

 

Bigirimana yeye ataanza kwa kucheza namba 7. Huyu ana kasi kubwa na kazi yake itakuwa kupeleka mashambulizi golini kwa wapinzani huku akipiga krosi safi kwa washambuliaji ni kati wa viungo washambuliaji bora hivi sasa Rwanda na namba 8 atacheza Fei Toto aliyepewa jina la fundi kutokana na utulivu wake na uwezo wa kupiga pasi safi zilizonyooka.

Namba 9 ni Kalengo ambaye ana sifa kubwa ya kukaa na mipira, pia kufunga kwa miguu yote miwili na kichwa, kazi kubwa wanayo mawinga Bigirimana na Sibomana katika kumpigia krosi safi na namba 10 ni Tshishimbi yeye kazi yake kubwa itakuwa ni kusaidia safu ya kiungo kwa kurudi chini kumsaidia Fei Toto kukaba na kuchukua mipira na kumpelekea Kalengo kwa maana ya kumpigia pasi za mwisho.

 

Winga wa kushoto ni Sibomana ambaye ana kasi kubwa na hatari akiwa na mpira kutokana na uwezo wake mkubwa wa kupiga chenga huku akiwa anakokota mpira na kupiga krosi safi kwa washambuliaji, pia ana sifa kubwa ya kupiga mipira ya adhabu nje na ndani ya 18 hivyo wapinzani wana kibarua kigumu.

ALI KIBA “NILIKUA Natamani ABDU KIBA Afunge MZUKA”

Comments are closed.