The House of Favourite Newspapers

Maisha ni yako, kwa nini mapenzi yakupe ‘stress’?

NI wiki nyingine tulivu kabisa tunakutana kupitia safu hii nikiwa na imani kwamba Mungu amekujaalia uzima na unaendelea na majukumu yako ya kila siku kama kawaida.  Mimi kama ilivyo ada yangu, namshukuru Mungu kwa kila jambo ambalo amekuwa akinitendea katika maisha yangu ya kila siku. Kikubwa nimshukuru kwa kunipa uwezo wa kuandika mambo ambayo yamekuwa ni yenye msaada kwa wengi walio kwenye uhusiano wa kimapenzi. Niseme tu kwamba, maisha yetu bila mapenzi hayajakamilika. Hata uwe mgumu vipi lakini kuna wakati utahitaji mwenza ambaye atayakamilisha maisha yako.

Ndiyo maana kila mmoja ana haki ya kupenda. Hakuna anayeweza kukushangaa kukuona umetokea kumpenda fulani kwa kuwa ni jambo linalokuja ‘automatikale’. Ukipenda umependa, huwezi kujizuia.

Lakini wakati ukweli ukiwa hivyo, leo nataka kuzungumzia jambo ambalo limekuwa likiwaweka wengi kwenye wakati mgumu. Ni kweli una haki ya kupenda lakini wataalam wa masuala ya mapenzi wanaeleza kuwa, hutakiwi kupenda kupita kiasi. Kumpenda mtu sana nako ni tatizo na ndiyo maana umekuwepo ‘ugonjwa’ unaoitwa KKK, yaani Kupenda Kupita Kiasi. Kama ni mfuatiliaji mzuri wa safu hii utakumbuka niliwahi kuuzungumzia ugonjwa huu kwa undani katika makala zilizopita.

Ukijaribu kufanya uchunguzi utabaini wapo watu ambao wanawapenda wapenzi wao mpaka wamechanganyikiwa. Hawa ni wale wanaofikia hatua ya kusema; ‘bila fulani siwezi kuishi’. Eti kwa sababu amempenda flani basi ikitokea ameachwa ni bora afe kuliko kuendelea kuishi, hii ni mbaya sana!

Ni mbaya kwa sababu wapo watu kweli waliofikia hatua ya kunywa sumu, kuchanganyikiwa na hata kushindwa kufanya shughuli zao kwa ufasaha kwa kuwa wametoswa.

Wakati mwingine hali inakuwa mbaya zaidi pale ambapo unamkuta mwanaume anampenda sana msichana flani wakati ameshaambiwa hapendwi. Licha ya kupewa jibu hilo bado anang’ang’ania kwa sababu tu amependa, hii siyo sawa hata kidogo.

Penda kwa kiasi, onyesha hisia zako kwa mtu ambaye unaamini atayafanya maisha yako yawe ni yenye furaha lakini ukiona unayempenda hana chembe za kukupenda, chukulia ni sawa kisha yaache maisha yako yaendelee. Hata kwa walio kwenye ndoa au uhusiano wa kawaida wanatakiwa kujizuia kupenda kupita kiasi na wala hawatakiwi kuonyesha kwamba ‘wamekufa na wameoza’. Kufanya hivyo ni kuingiza mizizi kwenye uhusiano ambao huna uhakika wa kudumu.

Ni wangapi unaowajua ambao walipenda kupita kiasi lakini leo hii wananyanyasika kama siyo kuachwa kabisa? Wapo wengi sana huko mtaani. Kimsingi kwa maisha ya sasa yalivyo, tunatakiwa kuwa makini katika kupenda kwa kuzingatia yafutayo; Kwanza, mpende yule anayeonesha kukupenda na hakikisha unamfanya aamini kwamba unampenda kutoka moyoni mwako. Pili, usikubali akutesa kisa umempenda. Ukiona analipiga teke penzi lako, chukulia kwamba umependa pasipo na penzi hivyo achana naye.

Tatu, hata kama unahisi kumpenda sanaaa, yeye ajue tu unampenda lakini si kuonesha kwa kiwango gani. Nne, zungumza na moyo wako na ‘uukontroo’ usipende sana. Madhara ya kupenda sana yanajulikana, upo? Ni hayo tu kwa leo, tukutane tena wiki ijayo.

Comments are closed.