The House of Favourite Newspapers

MBASHA AMAINDI INJILI KUTHAMINIWA MSIBANI

Emmanuel Mbasha

MSANII wa nyimbo za Injili, Emmanuel Mbasha ameonesha kutofurahishwa na kitendo cha nyimbo zao kupigwa nyakati za misiba tu kisha baada ya hapo hazithaminiwi na kwamba anatarajia kuitisha mgomo wa waimba injili wote Bongo. 

 

Akizungumza na Showbiz, Mbasha ambaye ni mlezi wa waimba injili alisema amefuatilia kwa muda mrefu na kubaini nyimbo zao zinathaminika nyakati za misiba tu tofauti na nyimbo za Bongo Fleva.

 

“Hivi karibuni tutakaa kikao ili tujadili hilo suala, kwa sababu nyimbo zetu hazithaminiwi kabisa, yaani zinapigwa tu siku ya Jumapili tena kwa masaa machache, hii maana yake nini?

 

“Ukija kuangalia siku za kawaida kuna media hazipigi kabisa nyimbo zetu ila nyimbo za kidunia ndio wamezipa sana kipaumbele, lakini siku za misiba ndio wanatukumbuka, eti utakuta nyimbo zetu ndio zinapigwa siku nzima, sasa si wapige hizo za kidunia ambazo wamezoea kuzipiga kila siku?

“Mungu hadhihakiwi bwana, sasa tutakaa kikao wanainjili wote ili tulijadili hili na ikiwezekana tugome ili nyimbo zetu ziwe zinachezwa muda wote sio siku za misiba tu,” alisema Mbasha.

Stori: Memorise Richard

Comments are closed.