The House of Favourite Newspapers

Mugabe Agoma Kwenda Bungeni Kuhojiwa Upotevu wa Trilioni 34

RAIS wa zamani wa Zimbabwe, Robert Gabriel Mugabe, amepuuza wito wa Bunge la nchi hiyo likimtaka afike mbele ya kamati yake inayochunguza mapato ya almasi. Mbunge anayeongoza kamati ya madini na nishati amesema Mugabe alikuwa amebakiwa na fursa moja tu ya kuripoti mbele ya kamati hiyo ili kujibu maswali husika.

 

“Tulimwandikia barua rais huyo wa zamani mara mbili ili aje lakini hakufanya hivyo, sasa tutamwandikia mara ya mwisho kama inavyotakiwa na sheria,” alisema Mbunge Themba Mliswa.

 

Uchunguzi huo ulioelezewa na gazeti la serikali la Herald kuwa unahusu upotevu wa Dola bilioni 15, (sawa na zaidi ya Tsh. Trilioni 34.2) unatafuta ufafanuzi kutoka kwa Mugabe kuhusu mapato ya almasi yenye thamani hiyo yaliyopotea wakati wa utawala wake.

 

Kamati hiyo imesema itatoa wito wa mwisho akitakiwa afike mbele yake Juni 11 mwaka huu. Wito wa kwanza ulimtaka afike mbele yake Mei 23 tatu asubuhi ambapo hakufika kutokana na kile alichosema Mliswa kwamba ilionekana haikuwa vyema kwa mtu wa umri wake kumtaka afike mbele ya kamati hiyo mapema asubuhi.

 

Alipoulizwa ni hatua gani zingechukuliwa iwapo Mugabe atakataa tena wito huo, Mliswa alisema akipuuza wito huo mara ya tatu, watatafuta msaada wa polisi. Wito wa pili ulikuwa afike kwenye kamati hiyo Mei 28 mwaka huu saa nane mchana lakini kiongozi huyo aliyeitawala nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 30, hakufika.

 

Mbali na kiongozi huyo aliyeondolewa madarakani Novemba mwaka jana, kamati hiyo imewaita mawaziri wa zamani, wa sasa na maofisa wa usalama waliohusika na uchimbaji wa almasi ili kupata ufafanuzi zaidi.

Comments are closed.