The House of Favourite Newspapers

Mwinyi Ataja Sababu Zilizomfanya Ajiuzulu Uwaziri

0

Rais mstaafu wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi ametaja sababu za kujiuzulu kwake nafasi ya Waziri wa Mambo ya Ndani kuwa kulitokana na kulinda heshima ya Taifa na ya Rais wa awamu ya kwanza.

Hata hivyo amesema anasikitika kuona chanzo cha kujiuzulu kwake bado hadi sasa kipo ambacho ni mauaji ya vikongwe jambo ni fedhea kubwa kwa Taifa kama Tanzania.

Akizungumza katika hafla ya siku ya wazee duniani leo Jumapili ambayo alikuwa mgeni rasmi, Mzee Mwinyi amesema hakuna haja kwa sasa kiongozi kujiuzulu kutokana na mauaji bali Serikali inapaswa kupambana na wauaji wote ili kutoruhusu hali hiyo kuendelea.

Mwaka 1976 akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwinyi alilazimika kujiuzulu nafasi yake baada ya kutokea mauaji katika Mkoa wa Shinyanga lakini miaka tisa baadaye akawa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kipindi cha miaka kumi.

“Hali ya kuongezeka kwa wazee ni jambo jema linaloonyesha Taifa linapata maendeleo lakini hili kuwaua vikongwe ni aibu na fedheha kubwa sana, naomba likomeshwe,” amesema Mwinyi

Kutokana na hali hiyo Mzee Mwinyi amevitwika jukumu kubwa vyombo vya habari akisema wakati wote atalia navyo kwa kuwa ndivyo vyenye jukumu la kutoa elimu kwa watu wenye tabia ya kuwaua vikongwe.

Awali Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema Serikali imetoa kipaumbele kwa wazee na haitasita kuwahudumia kila inapobidi.

Amesema Serikali inapeleka kila mwezi fedha katika kambi 17 za wazee huku ikiwa imeshanunua bajaji 10 kwa ajili ya kuwahudumia ikiwemo majiko matano ya kutumia.

Leave A Reply